2013-04-11 08:37:51

Vijana, jitahidini kutubu na kumwongokea Mungu katika ujana wenu! Wakati ni huu!


Baadhi ya vijana wenzetu wameuliza mara kadhaa iwapo tulikuwa hatuadhimishi imani kabla mpaka Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kuchukua hatua ya kuitisha mwaka wa imani. Kwa kweli tumekuwa tukiadhimisha imani na kuiishi tangu awali, tangu enzi za mababu. RealAudioMP3
Na pia si mara ya kwanza kuadhimisha mwaka wa imani. Kama utakumbuka zile enzi zetu vijana za mwaka 1967. Sasa usishtuke mapema juu ya nilikuwa wapi au ulikuwa wapi mwaka huo wa sitini na saba. Tulia usikilize ujumbe kwanza halafu baada ya kipindi ndio tuongelee siku za kuzaliwa. Halafu ukiwa katika hali hiyo hatuwezi kuelewana.
Naomba utulie kidogo tena rafiki yangu upate ung’amuzi wa mambo. Hili ndilo hema la vijana na nafasi yako ni hapo ulipo. Karibu sana studio za Radio Vatikani.
Mwaka 1967 Baba Mtakatifu Paulo wa sita alitiisha Mwaka wa imani. Aliuweka mwaka huo kuwa mwaka wa imani katika kumbukumbu ya karne 19 za tendo la kuifia dini mitume Petro na Paulo. Kijana hapa inafaa ujipime kuiona imani yako kwa kina. Je unawafahamu mitume hawa wawili, Petro na Paulo. Na je, unafahamu historia, imani na utume wao kadiri ya maandiko matakatifu na mafundisho ya Kanisa. Au huwa usomi hata Biblia. Lakini mi naamini kuwa huwa una soma.
Kwa ufupi tu ni kwamba mitume hawa waliacha vyote na kuamua kumfuasa Kristo na kutenda kazi ya uenezaji Injili. Mitume hawa wameanzisha jumuiya mbalimbali za kikristu kwa kuwafikishia watu habari njema na kuwabatiza kisha kuwaweka katika kuabudu kwa pamoja na kupendana. Waliwakumbushia imani ya dhati mara kwa mara jumuiya walizoanzisha, au walizokutana nazo pamoja na watu mbali mbali. Mitume hawa hawakukoma kufundisha na kuwaimarisha wenzao katika imani kwa kuwaandikia hata kwa kuwatembelea. Zaidi sana walikubali kwa hiari kuteseka na kufa kwa ajili ya imani yao kwa Kristu.
Huu ni mfano wa kuigwa kwako kijana. Iwapo mitume hawa katika umri wao ulivyokuwa umeenda waliamua kuongoka na kumfuasa Kristo kwa uaminifu, iwapo wao wameipigania imani na kuvumilia mateso mpaka kifo kwa ajili ya Kristo, kwa nini wewe kijana katika umri wako ushindwe. Kwanza sio kawaida yetu vijana wakristu kukata tamaa.
Baba Mtakatifu Paulo wa sita aliweka mwaka 1967 kwa lengo la kukualika wewe kuwa na wongofu wa ndani. Kuwa mtu wa toba, ujitakase na umuungame Mungu kwa uhakika na kwa uaminifu.
Mazingira tunamoishi leo ni tofauti sana na nyakati za mitume Petro na Paulo. Lakini imani tunayokiri na kuadhimisha ni ilele, haibadiliki. Wao walibuni mbinu za kufundisha, kuiungama na kuitetea imani hii. Kijana wa leo unao ufahamu na uwezo mkubwa unaoendana na maendeleo makubwa ya kijamii, sayansi na teknolojia. Tafadhali sana, tumia vipaji na taaluma ulivyonavyo ili kuishuhudia imani yako, ili kuiungama na kuiishi vema.
Katika umri ulionao, mazingira unamojikuta mara nyingi vinakupelekea kuanguka katika dhambi. Jitafakari kwa kina na ufanye toba ya kweli ndani kabisa ya nafsi yako. thamini, heshimu na adhimisha Sakramenti ya Upatanisho. Tubu dhambi zako sasa na kila unapoanguka dhambini. Mwaka huu wa imani jitahidi kuungama dhambi zako walau kila wiki.
Mbali ya dhambi kubwa na za mauti kuna dhambi zinazokuandama katika udhaifu wako. Mtakatifu Yohane asema “ukisema huna dhambi unajidanganya mwenyewe na kweli haitakuwemo ndani mwako”. Fanya toba, ungama dhambi. Jipatanishe nafsini mwako, jipatanishe na wengine na jipatanishe na Mungu. Uwe mtu wa kusamehe. Lakini pia chukua tahadhari ya kutokuanguka katika dhambi tena na chukua tahadhari usijeukatendwa vibaya. Bwana asema “uwe mpole kama njiwa lakini mwelevu kama nyoka”
Jitenge mbali na dhambi: tupia jela chuki na wivu; zipige shoti tamaa mbaya; ulevi na ulafi viunguze maji moto vizithubutu tena; weka maututi umbeya na uongo; udokozi, dhuluma na ulaghai tupia kwenye bwawa la mamba; weka kila aina ya uovu katika kaburi lisilo na tumaini la uzima. Jiaminishe kwa Kristu na Kanisa lake akuongoze na kukupatia utakaso, furaha, amani na ukarimu.
Tubu mtu wangu, tubu! Jitakase uwe huru! Radio Vatican itafanya sherehe kubwa pamoja na malaika wote wa mbinguni kila utakapokuwa unafanya ungamo la ndani na la kweli. Hii bahati ya pekee, hili jambo ni kubwa. Usilazie damu sherehe za wongofu namna hii. Ungama kwa dhati, badili maisha uselebuke pamoja na malaika. Na kama ukiniwahi hapa studio baada ya kuungama, sherehe hiyo gharama kwangu.
Mpaka wakati mwingine tena, ni sauti ya kinabii, Padre Celestine Nyanda.








All the contents on this site are copyrighted ©.