Baba Mtakatifu Francisko amemtumia salam za rambi rambi Askofu Franco Giulio Brambilla
wa Jimbo kuu la Novara, Italia kufuatia kifo cha Kardinali Lorenzo Antonetti, aliyefariki
dunia tarehe 10 Aprili 2013, akiwa na umri wa miaka 90. Enzi ya uhai wake aliwahi
kuwa Rais msimamizi wa rasilimali ya Vatican na mwakilishi wa Kipapa kwenye Kanisa
kuu la Mtakatifu Francisko wa Assisi.
Baba Mtakatifu anaungana na Jumuiya ya
Waamini wa Jimbo Katoliki la Novara, ndugu, Jamaa na wote walioguswa kwa msiba huu
mzito. Anasema, ni kiongozi aliyejitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya huduma kwa
Kanisa. Katika maisha yake, akakabidhiwa nyadhifa mbali mbali, kama Balozi wa Vatican
katika nchi mbali mbali duniani, Katibu mkuu wa Vatican.
Wakati wote huu ametoa
ushuhuda unaomwonesha kuwa kweli ni Padre mchapakazi na mwaminifu kwa Injili. Baba
Mtakatifu Francisko anachukua fursa hii kumwombea Marehemu Kardinali Lorenzo Antonetti,
pumziko la milele miongoni mwa wateule wake. Anawapatia baraka zake za kitume wote
wanaoomboleza msiba huu mzito.
Kardinali Lorenzo Antonetti alizaliwa tarehe
31 Julai 1922. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, akapadrishwa tarehe 26
Mei 1945. Baada ya kuhudumia Parokiani kwa takribani miaka minne, aliendelea na masomo
ya juu katika Chuo Kikuu cha Kipapa cha Mtakatifu Tomaso wa Akwino na kujipatia shahada
ya uzamivu katika sheria za Kanisa. Kunako mwaka 1949 hadi mwaka 1950 alijiunga na
Chuo cha Kipapa cha Diplomasia.
Kunako mwaka 1951 alianza utume wake wa kidplomasia
mjini Vatican: Akatumwa kufanya kazi Lebanon, Venezuela, baadaye akarudishwa mjini
Vatican kuwa mkuu wa kitengo cha uhusiano wa kimataifa. 1963 hadi mwaka 1967 alikuwa
mshauri kwenye Ubalozi wa Vatican nchini Ufaransa na mwaka 1968 akahamishiwa kwenye
Ubalozi wa Vatican nchini Marekani.
Baba Mtakatifu Paulo wa sita, tarehe 23
Februari 1968 akamteuwa Padre Lorenzo Antonetti kuwa Askofu mkuu na Balozi wa Vatican
nchini Nicaragua, utume ambao aliutekeleza hadi mwishoni mwa mwaka 1973. Akahamishiwa
Kinshasa, Zaire ya Zamani ambayo kwa sasa inajulikana kama DRC hadi mwaka 1977. Akahamishiwa
mjini Vatican na kuteuliwa kuwa ni Rais msimamizi wa rasilimali ya Vatican, hapa akapangiwa
majukumu mbali mbali na kunako mwaka 1983 alikuwa ni kati ya viongozi wa Kanisa waliohamasisha
kwa namna ya pekee uelewa na matumizi ya Sheria Mpya za Kanisa.
Askofu mkuu
Lorenzo Antonetti, tarehe 23 Septemba 1988 akateuliwa kuwa ni Balozi wa Vatican nchini
Ufaransa hadi mwaka 1995, alipoteuliwa kuwa Makamu wa Rais msimamizi wa rasilimali
ya Vatican, utume alioutekeleza hadi kufikia tarehe 5 Novemba 1998, alipoteuliwa na
Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa Pili kuwa Mwakilishi wa Kipapa wa Kanisa kuu la Mtakatifu
Francisko wa Assisi, hadi mwaka 2006.
Itakumbukwa kwamba, Baba Mtakatifu Yohane
Paulo wa pili, kunako tarehe 21 Februari 1998 alimteuwa kuwa Kardinali. Kwa kifo cha
Kardinali Lorenzo Antonetti, Dekania ya Makardinali kwa sasa ina jumla ya Makardinali
205, kati yao wenye haki ya kupiga na kupigiwa kura wakati wa mchakato wa uchaguzi
wa Khalifa wa Mtakatifu Petro ni 113 na wale wasiokuwa na haki ya kupiga wala kupigiwa
kura wamebaki 92.