2013-04-09 15:22:07

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa akutana na Papa Francisko mjini Vatican


Baba Mtakatifu Francisko, Jumanne tarehe 9 Aprili 2013 amekutana na kuzungumza na Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon alipomtembelea mjini Vatican. Mazungumzo ya viongozi hawa wawili yamedumu kwa takribani dakika ishirini. Viongozi hawa wawili wamejadili kuhusu: haki na amani; mafao ya wengi na haki msingi za binadamu.

Wamejadili kwa kina pia kuhusu vita, migogoro na kinzani zinazoendelea kujitokeza sehemu mbali mbali za dunia, lakini kwa namna ya pekee, Barani Afrika. Biashara haramu ya binadamu, tatizo na wakimbizi na wahamiaji ni kati ya mambo yaliyojadiliwa wakati wa mazungumzo ya viongozi hawa wawili pamoja na kuangalia jinsi ambapo Jumuiya ya Kimataifa inaweza kuzuia vita isitokee; umuhimu wa kujenga na kuimarisha mshikamano wa kimataifa pamoja na kuibua mikakati ya maendeleo endelevu. Baba Mtakatifu amebainisha pia mchango wa Kanisa katika ustawi na maendeleo ya binadamu sehemu mbali mbali za dunia.

Katibu mkuu aliambatana na ujumbe wa watu kumi na wawili waliopokelewa kwa gwaride la heshima walipowasili mjini Vatican. Katibu mkuu amemwambia Baba Mtakatifu Francisko kwamba, Umoja wa Mataifa na Vatican wanashirikisha malengo na mawazo kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya binadamu.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa akizungumza na waandishi wa habari amebainisha kwamba, hata Umoja wa Mataifa katika utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo ya Millenia unapania kupambana na baa la umaskini duniani kwa kuwajengea watu uwezo wa kupambana na hali yao ya maisha.

Katibu mkuu amesema, wamejadili kuhusu haki jamii na umuhimu wa kuongeza kasi ya kufikia Malengo ya Maendeleo ya Millenia. Amefurahishwa na azma ya Baba Mtakatifu Francisko kutaka kuwa ni daraja la Jumuiya mbali mbali za kiimani, ili kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano na uvumilivu kati ya watu.

Papa Francisko ni kiongozi wa amani mwenye malengo thabiti na kwa hakika ni sauti ya wanyonge. Katibu mkuu anasema amemkaribisha Baba Mtakatifu Francisko kutembelea Umoja wa Mataifa atakapopata nafasi katika ratiba zake.

Katibu mkuu amemzawadia Baba Mtakatifu Francisko kitabu ambacho kimeandikwa katika lugha sita zinazotumiwa na Umoja wa Mataifa katika mikutano yake. Baba Mtakatifu amempatia Katibu mkuu zawadi ya Picha ya Mji wa Roma na baadaye akawagawia Rozari Takatifu wajumbe waliokuwa kwenye msafara wa Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa.

Katibu mkuu pia amepata nafasi ya kukutana na kuzungumza na Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican pamoja na ujumbe wake. Kumbu kumbu zinaonesha kwamba, tangu uongozi wa Papa Yohane wa ishirini na tatu, Makatibu wakuu wa Umoja wa Mataifa saba wamekwisha kutembelea mjini Vatican na kuzungumza na Viongozi wa Kanisa.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa akiwa nchini Italia, amekutana na kuzungumza na Rais Giorgio Napolitano, Professa Mario Monti, Waziri mkuu wa Italia pamoja na Wakuu wa Bunge la Italia.







All the contents on this site are copyrighted ©.