2013-04-09 07:26:51

Fadhila ya unyenyekevu inajionesha kwa namna ya ajabu katika Fumbo la Pasaka


Unyenyekevu ni kanuni ya dhahabu inayomwezesha mwamini kukua na kukomaa katika fadhila ya imani, matumaini na mapendo kwa Mungu na jirani. Ni maneno yaliyosemwa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae Marthae, kilichoko mjini Vatican, Jumatatu, tarehe 8 Aprili 2013.

Ibada hii imehudhuriwa na wafanyakazi wa Sekretarieti ya Vatican pamoja na Masista wa Upendo waliorudia tena nadhiri zao za kitawa mbele ya Baba Mtakatifu Francisko. Anasema, historia ya maisha ya imani inafumbatwa kwa namna ya pekee katika hali ya unyenyekevu, kama inavyojionesha katika Fumbo la Umwilisho, Yesu, Nafsi ya Pili ya Fumbo la Utatu Mtakatifu alipoutwaa mwili na hatimaye kuzaliwa na Bikira Maria, katika mambo yote akawa sawa na binadamu isipokuwa Yeye hakutenda dhambi. Mwana wa Mungu alijinyenyekesha akawa mtii hata kukubali kuyamimina maisha yake pale juu Msalabani.

Huu ndio unyenyekevu uliooneshwa na Bikira Maria, aliyekubali mpango wa Mungu katika maisha yake, kama ilivyokuwa hata kwa Mtakatifu Yosefu, Baba Mlishi wa Mtoto Yesu.

Itakumbukwa kwamba, tarehe 8 Aprili, 2013, Mama Kanisa ameadhimisha Kumbu kumbu ya Siku kuu ya Bikira Maria kupashwa habari kwamba, atakuwa ni Mama wa Mungu. Mtakatifu Yosefu alijinyenyekesha mbele ya Mungu kiasi hata cha kudiriki kuchukua dhamana ya kuitunza Familia Takatifu sanjari na kuokoa maisha ya Bikira Maria na Mtoto Yesu yaliyokuwa hatarini, kielelezo cha unyenyekevu katika kuukubali mpango wa Mungu.

Baba Mtakatifu anasema, Mwenyezi Mungu ni mwingi wa huruma, upole na mnyenyekevu, fadhila ambayo imejionesha kwa namna ya ajabu katika maisha ya Yesu Kristo, Bikira Maria na Mtakatifu Yosefu, changamoto kwa Wakristo kujinyenyekesha ili kukua na kukomaa katika misingi ya imani, matumaini na mapendo.

Lengo ni kutoa fursa kwa mbegu ya upendo wa Mungu kuota na kukomaa katika hija ya maisha ya mwamini. Fadhila ya unyenyekevu katika upendo inajionesha kwa namna ya ajabu katika Fumbo la Msalaba: yaani mateso, kifo na ufufuko wa Kristo. Bila unyenyekevu, upendo utashindwa kutua nanga katika moyo na maisha ya mwamini. Baba Mtakatifu anahitimisha mahubiri yake kwa kuwaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kumwomba Mwenyezi Mungu ili aweze kuwakirimia fadhila ya unyenyekevu.







All the contents on this site are copyrighted ©.