2013-04-09 15:36:08

Changamoto kwa Nchi za Maziwa Makuu


Amani na utulivu katika eneo la Maziwa Makuu ni kati ya changamoto kubwa inayozikabili Tume za Haki na Amani katika nchi za Maziwa Makuu, Ukanda wa Afrika. Hii inatokana na ukweli kwamba, Ukanda huu mara kadhaa umekuwa ni uwanja wa vita na mauaji ya kimbari, mambo yanayokwamisha juhudi za kuleta haki, amani, upendo, mshikamano na maendeleo endelevu.

Kutokana na changamoto hizi, hivi karibuni, Tume ya haki na amani ya Jimbo Katoliki Kyangugu, ilifanya mkutano na wadau wa haki na amani Jimbo Katoliki la Bukavu, DRC.

Lengo la mkutano wa tume hizi kadiri ya habari kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki Rwanda ni kujaribu kupunguza hali ya kinzani inayoendelea kujitokeza baina ya nchi hizi mbili kiasi cha kutishia masuala ya usalama na amani katika eneo la Maziwa Makuu. Mkutano huu ulisimamiwa na kuongozwa na Askofu mkuu Fracois Xaver Maroy, wa Jimbo kuu la Bukavu, DRC na Askofu Jean Damascene Bimenyimana wa Jimbo Katoliki la Kyangugu, Rwanda.

Mkutano huu umehudhuriwa na Maparoko wanaohudumia Parokia za mpakani kati ya Rwanda na DRC, kwa pamoja walilenga kutafuta na kuendeleza mambo yanayodumisha misingi ya haki na amani pamoja na kudumisha uhusiano mwema kati ya wananchi wa nchi hizi mbili.

Hizi zote ni juhudi za kuhakikisha kwamba, waamini wanatolea ushuhuda wa imani yao katika matendo kama sehemu ya mchakato wa maadhimisho ya Mwaka wa Imani, unaokwenda sanjari na Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican pamoja na miaka 20 tangu Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili alipochapisha kwa mara ya kwanza Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki, muhtasari wa Kanuni ya Imani, Sakramenti za Kanisa, Maisha Adili na Maisha ya Sala.

Wajumbe wa mkutano huu kwa pamoja wameaziamia kwamba, Mapadre, Watawa na Waamini walei wajenge utamaduni wa kukutana mara kwa mara ili kujadiliana mambo msingi yanayowaunganisha kwa kushirikiana kwa karibu zaidi ili kuondoa dhana ya uadui na uhasama inayoendelea kujengeka miongoni mwa wananchi wa pande hizi mbili kiasi cha kutishia misingi ya haki, amani, utulivu na usalama katika eneo la Maziwa Makuu.

Kwa pamoja, wamedhamiria kuenzi utamaduni wa haki na amani na kwamba, vita ni mfumo ambao kwa sasa umepitwa na wakati, watu wanapaswa kujenga utamaduni wa kutafuta ufumbuzi wa matatizo na changamoto zao kwa njia ya majadiliano ya kina yanayoheshimu ukweli, uwazi upendo na mshikamano wa kitaifa, daima wakitafuta mafao ya wengi.








All the contents on this site are copyrighted ©.