2013-04-08 08:35:05

Siku ya kutetea utamaduni wa Injili ya Uhai


Mama Kanisa tarehe 8 Aprili 2013 anafanya Kumbukumbu ya Siku kuu ya Bikira Maria kupashwa habari kwamba, atakuwa ni Mama wa Mungu. Hii ni siku ambayo Mashirika mengi ya kutetea uhai wa mwanadamu yanaitumia kupinga utamaduni wa kifo unaoendelea kuku ana kupanuka kwa kasi ya ajabu sehemu mbali mbali za dunia. RealAudioMP3
Siku ya kutetea uhai ni mwaliko wa Kanisa kwa kushirikiana na watu wenye mapenzi mema kuendelea kuenzi Injili ya Uhai kama alivyobainisha Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili katika Waraka wake kichungaji, Injili ya Uhai.
Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania katika maadhimisho ya Siku ya Uhai Kimataifa, linawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kusimama kidete kulinda na kutetea zawadi ya maisha tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa Mama yake hadi mauti ya kawaida inapomfika kadiri ya mpango wa Mungu. Maaskofu wanakumbusha kwamba, maisha ya mwanadamu ni matakatifu na zawadi ya pekee kabisa kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
Hii inatokana na ukweli kwamba, maisha ya mwanadamu daima yanaonesha uhusiano na Mwenyezi Mungu ambaye ndiye Muumbaji. Kutokana na ukweli huu, kila tendo linalokwenda kinyume cha uhai wa mwanadamu ni jambo ambalo linapingana na haki na ukweli na hivyo ni kosa pia dhidi ya Mwenyezi Mungu.
Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania linawataka waamini, watunga sheria na sera kuhakikisha kwamba, wanathamini zawadi ya uhai tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake. Hii ni haki msingi kwa kila mwanadamu, inayopaswa kuheshimiwa na kuthaminiwa na wote.
Maaskofu wanakumbusha kwamba, hii si zawadi inayotolewa na Serikali kwa wananchi wake, bali ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu mwenyewe. Serikali zinawajibu wa kulinda na kutetea zawadi ya maisha dhidi ya utamaduni wa kifo, katika kila hatua yake ya maisha.
Kanisa linapenda kujenga na kuimarisha dhamiri nyofu ili watu watambue haki msingi za binadamu pamoja na umuhimu wa maadili na utu wema katika sheria na sera zinazotungwa na wanasiasa, ili ziweze kusimamia mafao ya wengi, utu na heshima ya binadamu. Vitendo vya utoaji mimba ni ukatili dhidi ya watoto ambao hawajazaliwa; watoto ambao wana haki zao msingi. Ni jukumu na dhamana ya Serikali kuhakikisha kwamba, inadumisha utamaduni wa uhai kwa watu wake.
Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania linasema, litaendelea kutoa huduma kwa Familia zinazokabiliana na hali ngumu ya maisha; huduma kwa wanawake wajawazito ili kuwasaidia kupokea na kutunza zawadi ya uhai kadiri ya mpango wa Mungu. Kanisa litaendelea kuwahudumia pia wanawake wanaokabiliwa na shinikizo la utoaji mimba kutoka katika Jamii, kwa kuwapatia msaada wa hali na mali, bila kusahau huduma kwa wanawake waliojifungua.
Ili kuweza kufanikisha sera na mikakati hii ya shughuli za kichungaji, kuna haja ya Kanisa kuwa na Mapadre, Watawa na Waamini walei walioandaliwa barabara ili kuweza kutekeleza utume huu nyeti kwa ajili ya huduma kwa Injili ya Uhai.








All the contents on this site are copyrighted ©.