2013-04-08 15:03:34

Mwenyeheri wa kwanza kutangazwa katika utume wa Papa Francisko


Kardinali Angelo Amato, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la kuwatangaza waamini kuwa wenyeheri na watakatifu, Jumapili iliyopita amemtangaza Cristoforo wa Mtakatifu Katarina aliyejulikana kwa wakati huo kama Cristoforo Fernàndez Valladolis aliyeishi kunako mwaka 1638 hadi mwaka 1690, mwanzilishi wa Shirika la Wahudumu wa Hospitali wa Yesu wa Nazareti kuwa Mwenyeheri.

Ibada hii imefanyika Jimboni Còrdoba, Hispania, baada ya kukamilika mchakato wa kumtangaza kuwa Mwenyeheri ulioanza kunako mwaka 1773 na hawamu ya kwanza kuhitimishwa Desemba 2012. kardinali Amato ametekeleza utume huu kwa niaba ya Baba Mtakatifu Francisko. Huyu anakuwa ni Mwenyeheri wa kwanza kutangazwa katika utume wa Papa Francisko.

Cristoforo Fernandès akiwa na umri wa miaka kumi alijiunga na Shirika la Ndugu Wadogo Wafransikani wa Mama Yetu wa Antigua, lakini hakuruhusiwa kukaa Shirikani humo na hivyo kumrudisha nyumbani kwao ambako Mama yake alikuwa anamsubiri kwa hofu na mashaka makubwa.

Akiwa nyumbani kwao, aliendelea na masomo, akakuza tasahufi ya toba na huruma kwa wagonjwa. Katika ujana wake, aliweza kutambuliwa na wengi kuwa ni mtawa aliyejitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya wagonjwa na wote waliokuwa wanateseka.Baada ya masomo na majiundo yake ya kitawa na Kipadre, akapadrishwa kunako tarehe 10 Machi 1663.

Kunako mwaka 1668 akaanza Shirika kwa ajili ya kuwasaidia wakulima waliokuwa wanakabiliana na hali ngumu ya maisha, baada ya tafakari ya kina, akatambua kwamba, Kristo alikuwa anamwalika kujitoa bila yakujibakiza kwa ajili ya maskini, wagonjwa na wazee, kiasi cha kuanzisha Shirika la kuwahudumia watu hawa kunako mwaka 1673.

Ni mtawa aliyeonesha weledi mkubwa katika masuala ya uongozi, utawala na usimamizi mzuri wa mali ya Kanisa, watu wakaonja upendo wa Mungu, kiasi kwamba, wakawa tayari kumpatia misaada kwa ajili ya maskini, kwani walimwamini kutokana na matumizi bora ya fedha walizokuwa wanampatia. Changamoto na uaminifu kwa mali ya Kanisa inayotolewa kwa ajili ya kuwasaidia maskini na wagonjwa.

Watu wengi nchini Hispania wakatambua ndani mwake imani, mapendo, huruma, ukarimu, moyo na bidii ya kazi, kwa wale wote waliobahatika kukutana na kuhudumiwa naye. Akiwa amechoka na kudhoofu kutokana na huduma kwa wagonjwa waliokuwa wamekumbwa na magonjwa ya mlipuko tarehe 24 Julai 1690 afariki dunia na akazikwa ndani ya Hospitali aliyoianzisha kwa mikono yake mwenyewe. Baadhi ya watawa wa Shirika lake, wanatekeleza utume wao Barani Ulaya na Afrika.







All the contents on this site are copyrighted ©.