2013-04-06 10:43:49

Waandishi wa habari Majimboni, tafuteni mbinu za kukabiliana na changamoto ya Uinjilishaji katika maeneo yenu!


Wafanyakazi kutoka katika Idara za Upashanaji habari za majimbo Katoliki DRC, kwa muda wa siku mbili kuanzia Ijumaa tarehe 5 hadi 6 Aprili 2013 wamepata fursa ya kukutanika na kujadili kwa pamoja changamoto wanazokabiliana nazo katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya nchini mwao, kwa kutambua na kuthamini mchango mkubwa unaotolewa na maendeleo ya sayansi na teknolojia katika mawasiliano ya Jamii.

Akizungumza katika mkutano huu, Padre Jean-Marie Bomengola, Katibu wa Idara ya Upashaji Habari, Baraza la Maaskofu Katoliki DRC, amewataka wadau hawa ambao wana mchango mkubwa katika mchakato wa Uinjilishaji kuhakikisha kwamba, wanatekeleza kwa ukamilifu mkubwa dhamana waliyokabidhiwa na Mama Kanisa katika Majimbo husika. Wanahabari kutoka Majimboni wanapaswa kujipanga vyema ili kukabiliana na changamoto za upashanaji habari zinazoendelea kuibuliwa na vyombo vya habari duniani.

Akizungumza kwa niaba ya Askofu Nicolas Djomo, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki DRC, Padre Felicien Mwanama, Katibu mkuu msaidizi wa Baraza la Maaskofu Katoliki DRC amewashukuru wajumbe kwa mchango wao mkubwa katika ulimwengu wa upashanaji habari.

Amewaalika kutumia mkutano wa wanahabari kutoka Majimboni kubadilishana uzoefu, ujuzi na mang'amuzi mbali mbali ili waweze kufanya maboresho makubwa katika idara za mawasiliano ya Jamii kutoka katika majimbo mbali mbali nchini DRC. Ni mwaliko wa kusoma alama za nyakati na kujibu matarajio ya waamini wanaowahudumia kwa njia ya vyombo vya mawasiliano ya Jamii.







All the contents on this site are copyrighted ©.