Papa Francisko: mwanadamu anapata ukombozi kwa Jina la Yesu Kristo
Mwanadamu anapata wokovu kwa jina la Yesu Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka
katika wafu na wala si kwa juhudi zake binafsi au maendeleo ya sayansi na teknolojia.
Ni maneno ya Baba Mtakatifu Francisko wakati wa mahubiri yake, Ijumaa ya Kipindi cha
Oktava ya Pasaka katika Ibada ya Misa Takatifu iliyofanyika kwenye Kikanisa cha Domus
Sanctae Marthae kilichopo mjini mjini Vatican na kuhudhuriwa na Watawa wa Shirika
la Fatebenefrateli pamoja na wafanyakazi wa Famasia ya Vatican.
Baba Mtakatifu
alikuwa anatafakari pamoja nao sehemu ya Matendo ya Mitume: 4: 1-12, kuhusu maana
na umuhimu wa Jina la Yesu, baada ya Mitume Petro na Yohane kukamatwa na kupelekwa
mbele ya Baraza kuu la Wayahudi, wakishambuliwa kwa kuulizwa ni kwa nguvu gani na
kwa jina la nani wameweza kufanya muujiza wa kumponya yule kiwete. Wao bila woga wala
wasi wasi wakajibu wakisema ni kwa Jina la Yesu Kristo, Jiwe lile walilokataa waashi
sasa limekuwa ni jiwe kuu la pembeni.
Yesu Kristo ndiye Mkombozi wa dunia,
ndiye anayeendelea kutenda miujiza miongoni mwa wafuasi wake. Jina la Yesu ambalo
limepigwa chapa mioyoni mwa waamini, linaendelea kuwaongoza katika safari ya maisha
yao ya kiroho.
Baba Mtakatifu anasema kwamba, hata muujiza uliofanywa na Mtume
Petro na wenzake walipoambiwa kutweka hadi kilindini bila ubishi ni mwendelezo wa
maajabu ambayo Yesu anafanya kwa njia ya mitume wake. Kuna uhusiano kati ya Yesu Kristo
na Roho Mtakatifu, kwani waamini wanaweza kuungama, kushuhudia na kuzungumza kuhusu
Jina la Yesu kwa njia ya Roho Mtakatifu, changamoto kwa waamini kuwa na imani thabiti
kwa Yesu Kristo anayeandamana pamoja nao katika hija ya maisha yao ya kila siku.
Kwa
mtu mwenye imani thabiti, anapolitaja Jina la Yesu anakuwa na nguvu ya kuweza kutekeleza
majukumu yake barabara, kwani anatambua uwapo na ulinzi wake madhubuti, kama alivyowahi
kusimuliwa na Mzee mmoja aliyekuwa amebahatika kupata watoto wanane katika maisha
yake. Kwa njia ya neema ya Ubatizo aliyoipokea aliweza kutekeleza wajibu wake kwa
kutambua kwamba anaye Yesu anayeandamana naye katika hija ya maisha yake! Ni mwaliko
wa kumtazama na kumtumainia Kristo Mkombozi wa dunia badala ya kuwakimbilia "wakombozi
uchwara" wanaojitokeza kila kunapokucha!
Baba Mtakatifu Francisko anaonya kwamba,
kwa waamini walio wengi, wanamkimbilia Yesu pale wanapokabiliwa na shida na magumu
ya maisha, lakini pale mambo yanapowaendelea sawa; Yesu hana nafasi tena katika maisha
yao na matokeo yake wanakimbilia kwa waganga wa kienyeji na wapiga ramli!
Waamini
kwa namna ya pekee wanachangamotishwa na Baba Mtakatifu Francisko kutolea ushuhuda
wa imani yao kwa Jina la Yesu Kristo Mkombozi wa dunia. Anawakumbusha waamini kwamba,
Bikira Maria anawasaidia kuwaonesha njia inayomwendea Yesu Kristo, lakini wajifunze
kutekeleza yale ambayo wanaambiwa na Yesu, kama ilivyokuwa wakati ule kwenye Harusi
ya Kana.
Mwishoni, Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini kujiachilia
mikononi mwa Jina la Yesu, ili waweze kupata kitulizo katika maisha yao ya kiroho!