2013-04-06 08:29:37

Dhibitini nyanyaso za kijinsia ili Kanisa liweze kuheshimiwa na kuthaminiwa linapotoa ushuhuda wake kwa walimwengu!


Baba Mtakatifu Francisko Ijumaa tarehe 5 Aprili 2013 amekutana na kuzungumza kwa kirefu na Askofu mkuu Gerhard Ludwig Muller, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Mafundisho Sadikifu ya Kanisa. Katika mazungumzo haya, Baba Mtakatifu aliweza kujulishwa masuala mbali mbali yanayohusika na Baraza hili la kipapa.

Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu Francisko amelitaka Baraza kuendeleza msimamo wa kushughulikia nyanyaso za kijinsia ndani ya Kanisa kadiri ya sheria, kanuni na maelekezo ambayo tayari yalikuwa yamekwishatolewa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita. Kanisa halina budi kuibua mbinu mkakati kwa ajili ya kulinda na kuwatetea watoto wadogo pamoja na kuhakikisha kuwa sheria inachukua mkondo wake dhidi ya watuhumiwa.

Jukumu hili linapaswa kutekelezwa na Maaskofu mahalia pamoja na Mabaraza ya Maaskofu Katoliki duniani. Lengo ni kuhakikisha kwamba, Kanisa linaendelea kuheshimiwa na kuaminiwa kwa njia ya ushuhuda na utume wake. Baba Mtakatifu Francisko anasema, wahanga wa nyanyaso za kijinsia wanapaswa kusaidiwa na Kanisa. Amewahakikishia sala zake, wale wote waliokumbwa na nyanyaso za kijinsia.







All the contents on this site are copyrighted ©.