2013-04-04 09:35:13

Umoja wa Mataifa katika harakati za kudhibiti biashara ya silaha kimataifa


Hatimaye, Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon amefurahishwa na ujasiri uliooneshwa na nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa kwa kuridhia Mkataba wa Udhibiti wa Biashara ya Silaha Kimataifa kwa kusema kwamba, huu ni ushindi wa Jumuiya ya Kimataifa. Mkataba huu utakuwa ni msaada mkubwa wa jitihada za Jumuiya ya Kimataifa katika kudhibiti vitendo vya jinai, mashambulizi ya kigaidi na chokochoko zinazoendeshwa na mababe wa vita sehemu mbali mbali za dunia.

Ni mkakati madhubuti unaopania pamoja na mambo mengine kulinda na kutetea haki msingi za binadamu hatua kubwa katika jitihada za Jumuiya ya Kimataifa za kupiga rufuku silaha za mahangamizi ambazo zimekuwa ni tishio kwa binadamu. Hizi ni juhudi na kampeni iliyofanywa usiku na mchana na vyama vya kiraia, anasema Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa.

Baraza kuu la Umoja wa Mataifa limepitisha Mkataba wa Kudhibiti Biashara ya Silaha Kimataifa kwa kuungwa mkono na nchi wanachama 154; Syria, Korea ya Kaskazini na Iran zilipinga muswada huu na nchi nyingine 23 hazikupinga wala kuukataa Muswada wa Mkataba huo ambao umepata baraka kubwa kutoka kwa Rais Barack Obama wa Marekani katika mchakato wa kudhibiti silaha nchini Marekani. Wachunguzi wa mambo wanasema, huu ni mkataba wenye nguvu, wenye uwiano mzuri na unaotekelezeka.

Mwanzoni, Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa alionesha masikitiko yake pale ambapo Mkataba huu ulipoanza kupingwa na Iran, Korea ya Kaskazini na Syria. Mkataba huu ambao unapongezwa na nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa, kwa mara ya kwanza unaweka vigezo vya kimataifa kwa ajili ya biashara ya silaha kimataifa; kwa kuzingatia haki msingi za binadamu pamoja na udhibiti wa silaha ndani ya nchi.

Wafanyabiashara wa silaha kimataifa watapaswa kuzingatia na kuheshimu vikwazo vya silaha vilivyowekwa kwa baadhi ya nchi; pale ambapo kuna vitisho vya mauaji ya kimbari pamoja na vita. Ni jukumu la kila nchi kupima na kuangalia ikiwa kama silaha zilizoko nchini mwake zinatumika katika masuala ya uvunjaji wa haki msingi za binadamu, vitendo vya kigaidi au makosa ya jinai.







All the contents on this site are copyrighted ©.