2013-04-03 11:45:17

Watawa waliotekwa nyara DRC Oktoba 2012 bado hawajaachiliwa


Baraza la Maaskofu Katoliki DRC kwa mara nyingine tena, limetoa wito kwa watu waliowatekwa nyara watawa watatu wa Shirika la Wasumption wa Mtakatifu Augostino tarehe 19 Oktoba 2012 kuwaachilia ili waweze kuendelea na maisha na utume wa kumtumikia Mungu na jirani zao.

Watawa walitekwa nyara kutoka katika Parokia ya Bikira Maria Mama wa Maskini, Jimbo Katoliki la Butembo-Beni na ambao hadi sasa hawajulikani mahali waliko. Hawa ni: Jean Pierre Ndulani, Anselme Wasinkundi na Edmund Bamutute. Maaskofu wanawaomba wateka nyara kuwaachilia mara moja watawa hao. Jitihada za kuwatafuta hadi sasa zinaonekana kugonga mwamba.

Maaskofu mara kadhaa wamewaomba wateka nyara kuwaachilia huru, kama walivyofanya pia Mababa wa Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya iliyofanyika mjini Vatican, mwezi Oktoba 2012 bila mafanikio. Maaskofu wanasema, bado hawajakata tamaa wanatumaini kwamba, watawa hawa wataweza kuachiliwa huru na hatimaye, kuendelea na utume wao!







All the contents on this site are copyrighted ©.