2013-04-03 09:41:37

Papa Francisko atembelea na kusali kwenye kaburi la Mwenyeheri Yohane Paulo II


Katika maadhimisho ya kumbu kumbu ya miaka minane tangu Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili alipofariki dunia, hapo tarehe 2 Aprili 2005, Baba Mtakatifu Francisko, Jumanne jioni, alikwenda kutembelea na kusali kwenye kaburi la Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili lililoko kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Sebastiani, ndani ya Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Katika ziara hii fupi, Baba Mtakatifu ameandamana na Kardinali Angelo Comastri, mhudumu mkuu wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro pamoja na Monsinyo Alfred Xuereb, katibu binafsi wa Papa Francisko.

Baba Mtakatifu alitumia fursa hii kwa ajili ya kusali kitambo na baadaye alitembelea na kusali kwenye makaburi ya Mwenyeheri Yohane wa Ishirini na tatu na Baba Mtakatifu Pio wa kumi. Hija hizi kwenye makaburi ya watangulizi wake zinalenga kwa namna ya pekee kuonesha mwendelezo wa maisha ya kiroho katika kumtukimia Kristo na Kanisa lake.

Ni mwelekeo huu pia ambao unajionesha kwenye uhusiano kati ya Baba Mtakatifu Francisko na Papa mstaafu Benedikto wa kumi na sita, wanapozungumza kwa faragha kwa njia ya simu.







All the contents on this site are copyrighted ©.