2013-04-03 12:14:24

Imarisheni imani yenu kwa Kristo Mfufuka na Kanisa lake ili muweze kuwa ni alama wazi ya ukuu wa maisha na matumaini dhidi ya ubaya, dhambi na kifo


Baba Mtakatifu Francisko, Jumatano, tarehe 3 Aprili 2013 aliendeleza Katekesi kuhusu Mwaka wa Imani, zilizokuwa zinatolewa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita kuhusu: Kanuni ya Imani: Siku ya Tatu Akafufuka kutoka katika wafu kadiri ya Maandiko Matakatifu.

Baba Mtakatifu anasema kwamba, Ufufuko wa Kristo ni kiini cha imani ya Kanisa, msingi wa matumaini ya utekelezaji wa ahadi za Mungu pamoja na ushindi dhidi ya dhambi na mauti. Mashahidi wa kwanza wa ufufuko wa Kristo walikuwa ni wanawake; waliosukumwa na upendo kwa Kristo kiasi kwamba, wakajihimu kwenda kaburini, huko wakapewa Habari Njema ya Ufufuko waliyowashirikisha Mitume.

Baba Mtakatifu anasema, hii ni changamoto kwa waamini kuweza kushirikisha ile furaha inayopata chimbuko lake kutoka kwa Kristo Mfufuka. Katika historia ya maisha na utume wa Kanisa, wanawake wamekuwa wepesi kuwafungulia wengine mlango wa imani kwa Kristo, kwani imani ni jibu makini la upendo.

Kwa njia ya jicho la imani, waamini pia wanayo bahati ya kukutana na Yesu Kristo Mfufuka na kuonja uwapo wake: katika Maandiko Matakatifu, Ekaristi Takatifu na Sakramenti mbali mbali za Kanisa; matendo ya huruma, wema na msamaha ni matukio ambayo yanaonesha uwapo endelevu wa Kristo katika hija ya maisha ya wafuasi wake hapa duniani.

Baba Mtakatifu Francisko anahitimisha Katekesi yake kwa kuwataka waamini, mahujaji na watu wenye mapenzi mema kuimarisha imani yao kwa Kristo Mfufuka ili waweze kuwa kweli ni alama wazi ya ukuu wa maisha na matumaini dhidi ya ubaya, dhambi na kifo.

Akizungumza na waamini na mahujaji katika lugha mbali mbali, Baba Mtakatifu Francisko kwa namna ya pekee, amewashukuru Vijana kutoka Lebanon walioshiriki katika kutunga na kuandika Tafakari ya Njia ya Msalaba kuzunguka Magofu ya Colosseo, Ijumaa kuu jioni.

Anawataka waamini kuongozwa na Mwanga wa Kristo Mfufuka, ili aweze kuwakirimia nguvu itakayowaletea mabadiliko ya ndani, ili waweze kuwa ni alama ya maisha yake duniani. Amewatakia wote amani ya Kristo mfufuka na kuwataka waguswe kwa namna ya pekee na upendo wa Kristo, ili kuutolea ushuhuda katika maisha adili.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini kutambua kwamba, Kanisa limezaliwa kutoka katika tumbo la Pasaka, mwaliko na changamoto kwa waamini kumtolea ushuhuda Yesu Kristo Mfufuka; kwa njia ya kuguswa na mahangaiko ya jirani, msamaha, upendo na huruma kwa wote. Furaha ya Kristo Mfufuka iwashukie na kukaa na familia zao.

Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu Francisko amemshukuru Kardinali Angelo Scola wa Jimbo kuu la Milani pamoja na mahujaji 10,000 kutoka Jimboni humo waliofika mjini Vatican kufanya hija, kama sehemu ya maandalizi ya kupokea Sakramenti za Kanisa kwa Vijana. Anasali na kuwaombea ili imani yao iweze kukua na kuongezeka na hatimaye, kuzaa matunda yanayokusudiwa. Anawataka vijana hawa kuongozwa na Injili ya Kristo, kama alivyofanya Mtakatifu Francisko wa Assisi.

Ni mwaliko wa kulisoma, kulitafakari na kuliishi katika hali ya unyenyekevu na ukawaida; katika hali ya udugu, huduma na matumaini mbele ya Mwenyezi Mungu na katika furaha ya kuwa na Baba ambaye yuko mbinguni anayewasikiliza na kuzungumza nao katika mioyo yao. Anawataka vijana kufuata dhamiri nyofu!







All the contents on this site are copyrighted ©.