Waamini 10,000 kutoka Jimbo Kuu la Milano wanafanya hija mjini Vatican
Kardinali Angelo Scola, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Milani, Italia anaongoza ujumbe
wa waamini elfu kumi kutoka Jimbo kuu la Milano ambao wako mjini Roma kwa ajili, kumshukuru
Mwenyezi Mungu kwa kulipatia Kanisa mchungaji mkuu, Baba Mtakatifu Francisko.
Jimbo
kuu la Milani ni kati ya Majimbo ya kwanza kabisa nchini Italia kufanya hija ya kichungaji
kwa ajili ya kumpongeza Baba Mtakatifu Francisko. Kundi hili la mahujaji kutoka Jimbo
kuu la Milani, limeanza hija yake hapo tarehe Mosi, Aprili na inatarajiwa kuhitimishwa
hapo tarehe 3 Aprili 2013 kwa kuhudhuria Katekesi ya Baba Mtakatifu Francisko.
Kuna
vijana elfu sita wenye umri wa miaka kumi na nne kutoka Parokia mbali mbali za Jimbo
kuu la Milani wanaojiandaa kupokea Sakramenti mbali mbali za Kanisa. Lengo kuu la
hija hii ya maisha ya kiroho kwanza kabisa ni kutaka kuimarisha imani yao kwa Kristo
na Kanisa lake, kwa kutembelea makaburi ya Viongozi wa Kanisa, kwa namna ya pekee,
Baba Mtakatifu Paulo wa sita, ambaye aliwahi kuwa ni Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Milani,
ambaye kwa sasa ameingizwa kwenye mchakato wa kutangazwa kuwa ni Mwenyeheri.
Jimbo
kuu la Milani, lilikuwa limepanga kuja Roma ili kumshukuru Baba Mtakatifu Benedikto
wa kumi na sita, kwa hija ya kichungaji aliyoifanya Jimboni mwao, wakati wa Maadhimisho
ya Siku ya Saba ya Familia Kimataifa.