2013-04-02 09:22:57

Ujumbe kwa Maadhimisho ya Siku ya 6 ya Ugonjwa wa Mtindio wa Ubongo Kimataifa


Askofu mkuu Zygmunt Zimowski, Rais wa Baraza la Kipapa la Wahudumu wa Sekta ya Afya, anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kuonesha moyo wa upendo na mshikamano kwa watoto wanaosumbuliwa na ugonjwa wa mtindio wa ubongo pamoja na familia zao, Jumuiya ya Kimatifa inapoadhimisha Siku ya sita ya Wagonjwa wenye mtindio wa ubongo duniani, tarehe 2 Aprili 2013.

Askofu mkuu Zimowski anabainisha kwamba, ugonjwa wa mtindio wa ubongo, licha ya maendeleo ya sayansi na teknolojia katika tiba, bado wagonjwa wanaendelea kuangaliwa kwa woga na unyanyapaa. Lakini ikumbukwe kwamba, wote hawa wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Tangu mwanzo, Kanisa limeonesha upendo na mshikamano wa pekee kwa watoto wenye mtindio wa ubongo kwa kuwapatia tiba na huduma msingi katika maisha yao.

Ni mwaliko wa kuendeleza upendo na mshikamano huu kwa wagonjwa na familia zao kwani hawa ni watu wanaotamani kuthaminiwa, kuonjeshwa furaha na matumaini; kupendwa na kuhudumiwa kikamilifu; kushirikishwa katika maisha na utume wa Kanisa, kwa kutambua kwamba, hata wao wanapaswa kuonjeshwa zawadi ya imani.

Kwa maneno machache, Askofu mkuu Zimowski anawataka waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuwa kweli ni Wasamaria wema, wakijitahidi kumwiga Kristo, kielelezo makini cha Msamaria mwema, kwani kwa njia ya mateso, kifo na ufufuko wake ameweza kuukomboa ulimwengu.

Kanisa linapofanya kumbu kumbu ya miaka minane, tangu alipofariki dunia Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili, hapo tarehe 2 Aprili 2005, Kanisa linawaweka wagonjwa wote wa mtindio wa akili chini ya maombezi ya Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili, aliyekezia kwamba, ubora wa maisha ya Jamii yoyote ile unapimwa kwa jinsi gani Jamii inajitosa kimaso maso kuwahudumia wanyonge na wale wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii; kwa kuheshimu na kuthamini utu wao kama binadamu walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Haki zao zinapaswa kuheshimiwa na kwamba, licha ya ulemavu wanaokabiliana nao, wanapaswa pia kushirikishwa katika uhalisia wa maisha, kwa kuwapatia fursa ya kuchangia vipaji walivyokirimiwa na Mwenyezi Mungu. Kwa njia hii anasema Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili, Jamii itakuwa inatembea katika sheria na haki.

Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kuwaalika waamini na watu wenye mapenzi mema kuhakikisha kwamba, waamini wanashirikiana kuzima kiu ya undani wa maisha yao, kwa kuwa na mwono sahihi wa binadamu badala ya mwanadamu kugeuka na kuwa kama bidhaa, jambo ambalo ni hatari kwa nyakati hizi.

Ni matumaini ya Askofu mkuu Zygmunt Zimowski kwamba, waamini na watu wenye mapenzi mema wataungana kwa pamoja ili kuwaonjesha upendo na mshikamano watoto wanaokabiliwa na ugonjwa wa mtindio wa ubongo.







All the contents on this site are copyrighted ©.