2013-04-02 08:43:50

Rais Uhuru Kenyatta anatarajiwa kuapishwa rasmi hapo tarehe 9 Aprili 2013


Wananchi wa Kenya wanasema, mchakato wa uchaguzi umekwisha na Rais Uhuru Kenyatta ameshinda kihalali, sasa wananchi wa Kenya wanapaswa kuunganisha nguvu zao kwa ajili ya kujenga uchumi wa nchi. Rais Uhuru Kenyatta aliyeshinda uchaguzi mkuu dhidi ya mpinzani wake mkuu Raila Odinga anatarajiwa kuapishwa kuwa Rais wa Kenya hapo tarehe 9 Aprili 2013, kadiri ya taarifa zilizotolewa na Shirika la habari la Reuters.

Jeshi la Polisi nchini Kenya limekwishawatia pingu watuhumiwa 23 waliokuwa wanajihusisha na uchochezi na vurugu hivi karibuni mara baada ya Mahakama kuu ya Kenya kutangaza kwamba, Rais Uhuru Kenyatta alikuwa ameshinda kwa kupata kura halali. Wananchi wa Kenya wanaendelea kuhimizwa kulinda na kudumisha haki na amani na kwamba, vurugu, chuki na uhasama havina nafasi tena, kwa watu wanaoitaka kucharuka kwa maendeleo kwa sasa.

Pamoja na hali ya amani na utulivu kurejea tena katika maeneo mbali mbali nchini Kenya, lakini, Mombasa bado hali si shwari sana kutokana na baadhi ya wananchi kuendeleza azma ya kutaka kujitenga kutoka Kenya. Hii ni kutokana na matatizo ya ardhi na hali mbaya ya kiuchumi wanayokabiliana nayo wananchi wa eneo hili.







All the contents on this site are copyrighted ©.