Imegota miaka 8 tangu alipofariki dunia Papa Yohane Paulo II
Mama Kanisa anafanya kumbu kumbu ya miaka minane, tangu Mwenyeheri Yohane Paulo wa
Pili alipofariki dunia kunako tarehe 2 Aprili 2005, baada ya kufanya hija ya maisha
ya kiroho, akiubeba Msalaba wake na kuendelea kumfuasa Kristo aliyeteswa, akafa na
kufufuka kutoka katika wafu. Kardinali Jorge Mario Bergoglio, ambaye kwa sasa ni Baba
Mtakatifu Francisko, aliteuliwa na Papa Yohane Paulo wa Pili kuwa Askofu kunako mwaka
1992 na mwaka 2001 akamteuwa kuwa Kardinali.
Kardinali Bergoglio akihubiri
katika Ibada ya Misa Takatifu, Mei Mosi 2011, kwenye Kanisa kuu la Buenos aires, Argentina,
wakati Mama Kanisa alipokuwa anamtangaza Mtumishi wa Mungu Yohane Paulo wa Pili kuwa
Mwenyeheri, alisema kwamba, Kanisa lilikuwa linashangilia na kumtukuza Mwenyezi Mungu
kwa zawadi kubwa ya Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili.
Ni kiongozi aliyeonesha
ujasiri wa pekee katika kupambana na mifumo kandamizi, akawaimarisha ndugu zake katika
imani kwa njia ya hija zake za kichungaji, lakini zaidi kwa njia ya ushuhuda wa maisha
yake; ushuhuda amini wa Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu! Mwenyeheri
Yohane Paulo wa pili alitumaini kwa namna ya pekee huruma ya Mungu katika maisha na
utume wake. Alithubutu kuwaalika waamini kuondokana na woga na badala yake wamfungulie
Kristo malango ya mioyo yao!
Kardinali Bergoglio wakati akiadhimisha kumbu
kumbu ya miaka miwili tangu alipokuwa amefariki dunia Papa Yohane Paulo wa pili alisema,
kwa hakika, alikuwa ni kielelezo cha umoja wa Watu wa Mungu; Mtu wa sala, aliyetumia
muda wake mwingi kwa ajili ya kusali na kuabudu Ekaristi Takatifu, mambo yaliyomkirimia
nguvu ya maisha ya kiroho kuweza kusonga mbele kwa imani na matumaini.
Ni
kiongozi aliyejitahidi kutekeleza mapenzi ya Mungu katika maisha yake. Mwenyeheri
Yohane Paulo katika maisha na utume wake amekuwa kweli ni shahidi amini wa Kristo
na Kanisa lake.