2013-04-01 08:57:57

Fadhila za familia ya kikristo!


Katika mwaka huu wa imani, Kanisa linaitazama familia kwa namna ya pekee kama kitalu cha pekee kwaajili ya uinjilishaji wa kina katika jamii zetu. Ni katika familia tunapata viongozi mbalimbali wa Kanisa na Taifa kwa ujumla. Kama familia zetu hazijakuwa katika misingi bora ya kimaadili ni wazi kuwa huo ni mwanzo na chanzo cha mmomonyoko wa maadili katika jamii. RealAudioMP3
Wahenga wetu walikuwa na misemo na methali nyingi ambazo ukizitafakari kwa kina zina mafunzo mengi katika jamii yetu ya leo. Methali ambayo imenijia mara akilini mwangu ni hile isemayo “Mtoto umleavyo ndivyo akuavyo”. Kama familia zetu hazina maadili mema, tutegemee pia kupata viongozi wetu katika Nyanja zote wasiokuwa na maadili mazuri.
Maadili mema ni fadhila inayokua na kutengeneza mizizi katika maisha yetu sisi binadamu pale yanapofanyiwa kazi. Hivyo ni dhairi kuwa kama familia zetu hazijajengeka katika misingi bora ya upendo na utu mwema, hatuwezi kuwa na taifa lenye watu wenye kupendana, kujaliana na kuthaminiana.
Katika mwaka huu wa imani sisi wanafamilia tunaalikwa na Mama Kanisa kutafakari kwa namna ya pekee mafundisho ya Kanisa kuhusu maisha ya familia na changamoto mbalimbali tunazo kabiliana nazo. Tumshukuru Mungu kwa zawadi ya chombo hichi cha Kanisa ambacho mara kwa mara kimekuwa na lengo la kutuongoza kwenye kweli za maisha kwa lengo la kutaka kutuongoza vema kuelekea kwa muumba wetu. Tukitumia zawadi hii vyema kamwe hatuwezi kupotea kwani Kristu mwenyewe ameahidi kuwa na Kanisa lake “siku zote, hata ukamilifu wa dahari (Mt. 28:20)
Katika Mtaguso wa Pili wa Vatikani katika Konstitusio ya kichungaji juu ya Kanisa katika ulimwengu wa leo Mababa wa Mtaguso walitafakari maisha ya ndoa na familia kwa kina na kutoa sura moja nzima kwaajili ya kujadili maisha ya ndoa na familia na changamoto mbali mbali tunazo kabiliana nazo katika ulimwengu wetu wa leo. Sauti na busara za Mababa wa Mtaguso huu zinaendelea kuzungumza nasi katika maisha yetu ya kila siku.
Baadhi ya changamoto zilizotolewa katika mtaguso huo ni kuhusu tatizo la talaka, mitala, maisha ya mume na mke nje ya ndoa na changamoto nyingine nyingi tunazokabiliana nazo. Mtaguso huo ulikuwa unafahamu wazi umuhimu wa ndoa na maisha ya familia katika maisha ya Kanisa na ulimwengu kwa ujumla.
Hivyo basi, wakati wa mkutano wa Mtaguso ulikuwa wakati wa pekee wa kuweza kuyamulika matatizo hayo kwa mwanga wa Injili. Jambo hilo lilifanyika kwa kuelezea kwa kina maana ya ndoa na familia kutokana na uelewa wa Kanisa ambao msingi wake ni ufununuo wa Kimungu kutoka katika Maandiko Matakatifu.
Hatuwezi kuzungumzia maisha ya familia bila kugusa maisha ya ndoa kwasababu ndoa ndio inayotengeneza maisha ya familia. Katika siku hii ya leo ningependa tutafakari kwa pamoja kuhusu ndoa kama ushirika wa maisha yote kati ya mume na mke na kadiri tutakapokuwa tunaendea kuitafakari mada yetu tutaweza pia kutafakari jinsi ushirika huu ulivyoanza.
Mwalimu wangu wangu alinifundisha kuwa ninaposoma kwaajili ya kujiandaa na mitihani niandae ufupisho au muhtasari wa kile ninachokisoma kusudi niweze kukumbuka kiuraisi. Tunaweza kutoa maelezo mengi kuhusu manna ya ndoa lakini katika maelezo yote tunaweza kupata sentensi fupi ya ufupisho inayoweza kutupa maana ya ndoa. Tunaweza kuielezea ndoa kwa ufupi kama ushirika wa maisha yote kati ya mume na mke.
Tukisoma sharia za Kanisa kifungu cha 1055 tunaweza kupata maelezo mazuri sana kuhusu maana ya ndoa. Kifungu hiko kinaelezea ndoa kama agano kati ya mume na mke wenye lengo la kutengeneza ushirika wa kudumu na ushirika huu unajengwa katika msingi wa upendo kati ya wenzi wawili, kushiriki katika kazi ya uumbaji na kuhakikisha kuwa zawadi ya watoto watakaojaliwa wanapata elimu bora itakaowasaidia kukua katika misingi bora ya kimaadili.
Katika uelewa wa ndoa katika Kanisa kuna vipengele viwili ambavyo siku zote inabidi kuvikumbuka, navyo ni hivi: ndoa inayotambulika kikanisa, inatengeneza umoja usioweza kutenganishwa na binadamu yeyote.
Katika tafakari yetu ya leo na tunavyoendelea kuutafari mwaka huu wa imani. Tuziombee familia zote zilizo katika utengano na magomvi ya hapa na pale kusudi upendo wa Mungu ukapate kuzishukia, zikapate kuunganika tena na zile zilizokuwa na ugomvi zikapate kuwa na maelewano.
Makala hii imeandaliwa na Shemasi Titus Nkane OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.