Adhimisho la Fumbo la Pasaka ni chemchemi ya furaha, amani upendo na mshikamano wa
dhati!
Patriaki Fouad Twal wa Yerusalemu, katika mahubiri yake kwenye Maadhimisho ya Siku
kuu ya Pasaka, yaliyofanyika kwenye Kaburi Takatifu la Yesu mjini Yerusalemu, hapo
tarehe 31 Machi 2013, amewatakia waamini na watu wote wenye mapenzi mema Pasaka yenye
kheri na baraka tele katika maisha yao! Maadhimisho ya Fumbo la Pasaka ni chemchemi
ya furaha ya kweli, amani, upendo na matumaini mapya yanayobubujika kutoka kwa Kristo
Mfufuka.
Kaburi wazi ni kielelezo cha imani kwa Kristo mfufuka, imani ambayo
waamini wanapaswa kuirutubisha kwa kujenga na kuimarisha uhusiano mwema na Mwenyezi
Mungu, kwa njia ya Sala, Tafakari ya Neno la Mungu na ushuhuda wa matendo ya huruma,
hasa kwa wanyonge na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Ufufuko wa Kristo ni
kiini cha Imani ya Wakristo, changamoto ya kuendeleza umoja na majadiliano ya kiekumene,
ili siku moja waweze kuwa chini ya Mchungaji na Imani moja.
Maadhimisho ya
Mwaka wa Imani, kiwe ni kipindi cha kukabiliana na changamoto mbali mbali za kiimani
kwa ujasiri na matumaini mapya. Changamoto zilizoko mbele ya waamini kwa wakati huu
ni pamoja na: Uinjilishaji mpya unaopaswa kujipambanua kwa njia ya huduma kwa maskini
na ushuhuda wa nguvu ile ya upendo wa Kristo inayotenda kazi ndani mwao kama anavyofanya
kwa sasa Baba Mtakatifu Francisko. Kuchaguliwa kwake ni zawadi ya Roho Mtakatifu kwa
watu wa nyakati hizi.
Mchakato wa Uinjilishaji Mpya anasema Patriaki Twal unajikita
hasa katika hija ya pamoja inayofanywa na waamini, huku wakidumisha udugu, umoja,
upendo na mshikamano wa dhati; daima wakijitahidi kutembea katika Mwanga wa Kristo
Mfufuka. Kanisa la Mwanzo lilijengeka na kuimarika kwa njia ya Maadhimisho ya Fumbo
la Ekaristi Takatifu pamoja na Tafakari ya kina ya Neno la Mungu inayomwilishwa katika
matendo ya huruma, changamoto ya kuendeleza mshikamano wa kidugu, hata kiasi cha kujitoa
bila ya kujibakiza kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake.
Kanisa Mashariki ya
Kati linateseka na kukabiliwa na changamoto na fursa mbali mbali zinazoweza kupata
majibu ya kina kwa njia ya ushuhuda wa imani. Waamini waendelee kuonesha mshikamano
na wakimbizi, wahamiaji na wote wasiokuwa na makazi maalum kutoka Syria na nchi ambazo
bado kinzani na migogoro ya kijamii inaendelea kufuka moshi. Pasaka ya Kristo Mfufuka
iwe ni chemchemi ya furaha kwa Wakristo wote hata katika shida na mahangaiko yao ya
kila siku. Hata baada ya Ufufuko wa Kristo, bado waamini wataendelea kubeba na kuandamana
na Misalaba ya Maisha yao kwa imani, matumaini na mapendo.
Waamini wanachangamotishwa
kwa namna ya pekee, kama alivyosema Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita,
kuinua macho yao juu ya Msalaba wa Kristo, ili wapate kumwona na kumshuhudia Yesu
Kristo, Nafsi ya Pili ya Fumbo la Utatu Mtakatifu. Anaonesha ubinadamu na umungu wake,
chemchemi ya matumaini ya Kikristo!
Patriaki Twal anasema katika mahubiri
yake kwamba, ana uhakika mkubwa kwamba, Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na
sita, licha ya kusali na kutafakari kwa ajili ya Kanisa, ataendelea pia kuombea: misingi
ya haki, amani na upatanisho katika Nchi takatifu. Amehitimisha mahubiri yake ya Siku
kuu ya Pasaka kwa kuwatakia watu wote amani na Pasaka Njema.