Ushuhuda wa wanawake, kaburi wazi na kumbu kumbu endelevu ya uwepo wa Kristo Mfufuka
ndicho kiini cha ujumbe wa Kesha la Pasaka 2013
Baba Mtakatifu Francisko katika Kesha la Pasaka, kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro
mjini Vatican, amekazia mambo makuu matatu: dhamana ya wanawake katika ushuhuda wa
imani na upendo wao kwa Kristo; Kaburi wazi, tukio ambalo limeleta mabadiliko makubwa
katika historia ya mwanadamu na changamoto kwa waamini kuendelea kufanya kumbu kumbu
ya mateso, kifo na ufufuko wa Kristo.
Baba Mtakatifu Francisko, anasema, Mwijili
Luka anawaonesha wanawake waliokwenda kaburini wakiwa na manukato kwa ajili ya kuupaka
mwili wa Yesu. Ni kitendo cha huruma na upendo wa dhati kwa Yesu, ambaye kwa namna
ya pekee, katika maisha na utume wake, aliwapatia changamoto ya kumfuasa, wakamsikiliza
na kutambua kwamba, kwa hakika alikuwa ameuinua utu na heshima yao, ndiyo maana walimfuata
katika Njia ya Msalaba hadi Mlimani Kalvari, wakaona mahali alipozikwa.
Kifo
cha Kristo ingawa kiliacha huzuni na majonzi makubwa kwa wanawake hawa, lakini kamwe
hakikuzima upendo uliowasukuma kwenda kaburini alfajiri na mapema, walipofika wakapigwa
na bumbuwazi kwa kuona Kaburi wazi, jambo ambalo liliwaachia maswali magumu vichwani
mwao, wakitaka kufahamu maana ya tukio hili.
Baba Mtakatifu Francisko anasema,
upya wa maisha unaoletwa na Mwenyezi Mungu, wakati mwingine unawaogofya wanawadamu.
Kama ilivyokuwa kwa mitume wa Yesu, walijifungia katika undani wao, wakitafuta usalama
na uhakika wa maisha! Kimsingi mwanadamu anaogopa kushangazwa na Mwenyezi Mungu, changamoto
kwa waamini kumwachia nafasi Mungu aweze kuwakirimia upya wa maisha.
Hii inatokana
na ukweli kwamba, mara nyingi waamini wanachoka, wanakata tamaa na kuonja uzito wa
dhambi zao, kiasi cha kujiuliza ikiwa kama wanaweza kweli kukabiliana na magumu pamoja
na changamoto zote hizi? Baba Mtakatifu anawaalika waamini kuhakikisha kwamba, hawajifungi
katika undani wao, wala kupoteza imani na hatimaye, kukata tamaa, kwani Mwenyezi Mungu
anaweza kumletea mwanadamu mabadiliko sanjari na kumsamehe dhambi zake, ikiwa kama
mwamini atakimbilia huruma na upendo wake.
Mwinjili Luka anawaonesha wanawake
waliokuwa wanamtafuta Yesu aliyekuwa amefufuka kati ya wafu, lakini wanaambiwa hayupo
hapo amefufuka. Ufufuko wa Yesu ni tukio ambalo limeleta mabadiliko makubwa katika
maisha ya waamini na ulimwengu kwa ujumla. Yesu Kristo amefufuka, Yu hai, anaishi
kwa wakati huu na kuwaelekeza wafuasi wake kwa siku za usoni.
Huu ndio upya
wa maisha unaoletwa na Mwenyezi Mungu, yaani ushindi dhidi ya dhambi na mauti pamoja
na mambo yote yanayofisha utu na heshima ya binadamu, changamoto kwa waamini kuongozwa
na upendo, wanapomtafuta Yesu katika hija ya maisha yao.
Matatizo na changamoto
za maisha, zisiwafanye kujikuta wanatumbukia katika huzuni na simanzi kwani kwa kufanya
hivi watakabiliana na kifo, kiasi cha kushindwa kumtafuta Yesu ambaye amefufuka. Baba
Mtakatifu Francisko anawaalika waamini kumkubali na kumpokea Yesu ili aweze kuingia
katika maisha yao wakimpokea kwa imani kama rafiki yao. Kama kuna mwamini aliyejisikia
kuwa mbali na Yesu, akumbuke tu kwamba, Yesu bado anaendelea kufungua mikono yake
kuonesha kwamba yuko tayari kumpokea kwa mikono miwili.
Kwa wale wanaoona
shida na kigugumizi cha kumfuasa, wanaalikwa kupiga moyo konde kwani kwa hakika hataweza
kuwalaghai, kwani daima yuko karibu na kuwakirimia amani ili waweze kuishi kama anavyotaka
Yesu.
Baba Mtakatifu Francisko anasema kwamba, wanawake walibahatika kukutana
na upya uliokuwa umeletwa na Mwenyezi Mungu: Yesu alikuwa amefufuka na ni mzima. Baada
ya kusikiliza kwa makini ujumbe juu ya Kristo Mfufuka, walioweza kuupokea kwa imani
kubwa, wakikumbushwa kwamba, ilikuwa imempasa Mwana wa Adamu, kutiwa mikononi mwa
wenye dhambi, kusulubiwa na hatimaye siku ya tatu kufufuka kutoka katika wafu.
Changamoto
kwa waamini ni kufanya kumbu kumbu endelevu ya mkutano wao na Yesu, Maneno na Matendo
yake, lakini zaidi wakumbuke kwa njia ya mapendo mang'amuzi ya Kristo Mwalimu na Bwana,
yaliondoa wasi wasi na woga hata wakadiriki kujitosa kimaso maso kwenda kuwapasha
habari mitume juu ya ufufuko wa Kristo. Hii ni hija ya hatari anasema Baba Mtakatifu
Francisko. Ni tukio linalofungua moyo ili kuweza kupokea matumaini kwa ajili ya kesho
iliyo bora zaidi. Waamini waendelee kujifunza kumbu kumbu endelevu ambayo mwenyezi
Mungu ametenda katika maisha yao,
Mwishoni, Baba Mtakatifu Francisko anawakabidhi
waamini chini ya maombezi ya Bikira Maria aliyebahatika kuyahifadhi matukio yote haya
moyoni mwake; wamwombe Bwana yesu ili awajalie kushiriki katika Ufufuko wake, unaowakarimia
waamini mabadiliko na maisha mapya. Waamini wafanye kumbu kumbu endelevu kwa kile
ambacho Mwenyezi Mungu anachotenda katika historia ya kila mwamini na dunia katika
ujumla wake; wamwone na kujisikia kuwa yu katikati yao, daima wamtafute Yesu aliyefufuka
ambaye ni mzima!