Sanda takatifu ni kielelezo cha hali ya juu cha huruma na upendo wa Mungu uliomwilishwa
katika historia
Baba Mtakatifu Francisko ametuma ujumbe kwa Askofu mkuu Cesare Nosiglia wa Jimbo kuu
la Torino, katika Ibada ya Kuabudu Sanda Takatifu ya Yesu. Anasema, kwa njia ya maendeleo
ya sayansi na teknolojia ya mawasiliano, leo hii waamini wanaweza kushiriki katika
tukio hili la imani. Hata katika mazingira kama haya anasema, Baba Mtakatifu Francisko,
waamini hawaweze kusimama hivi hivi tu, bali wanapaswa kuonesha heshima na ibada.
Hii ni Sanda inayoonesha uso wa mtu aliyefariki dunia, lakini bado anaendelea
kuwatazama waja wake katika hali ya ukimya na kutoka katika undani wao, anaweza tena
kuzungumza nao! Ni Jambo la ajabu kuona kwamba, waamini kutoka sehemu mbali mbali
za dunia, wamekwisha kupata fursa ya kusimama na kufanya tafakari ya kina kuhusu Mtu
huyu alisulubiwa na kufa juu ya Msalaba.
Sanda Takatifu ni mwaliko kwa waamini
kufanya tafakari ya kina kuhusu Yesu wa Nazareti. Sura iliyochapwa kwenye Sanda Takatifu
ni mwaliko kwa waamini kukwea kwenda Mlimani Kalvari, ili kuutafakari Mti wa Msalaba,
unaoonesha katika ukimya fadhila ya upendo.
Baba Mtakatifu Francisko anawaalika
waamini kujiruhusu ili waguswe na macho yanayopenda kutoka katika Sanda Takatifu.
Katika hali ya ukimya, wasikilize kwa makini yale ambayo Yesu anataka kuwashirikisha
nje ya kifo chake. Sanda hii ni kielelezo cha hali ya juu kabisa cha upendo wa Mungu
uliofanyika Neno; Na Neno akafanya Mtu na kuzaliwa katika historia, kielelezo cha
upendo na huruma ya Mungu kwa waja wake, kiasi kwamba, aliweza kujitwalia juu yake
maovu na dhambi za binadamu, ili aweze kuwakomboa kutoka katika lindi la dhambi na
mauti.
Uso unaoonekana kwenye Sanda Takatifu wa mtu ambaye amekabiliwa na
mateso makali ni kielelezo makini cha wale wote ambao utu na heshima yao havithaminiwi
tena; wanaendelea kukabiliana na vita na uvunjifu wa haki msingi za binadamu bila
kusahau mateso ya maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.
Ni Uso
unaoonesha pia amani na utulivu wa ndani wa mtu ambaye kwa hakika alikuwa na ujasiri
mkubwa, changamoto ya kuendelea kuimarisha imani bila kupoteza matumaini na upendo
wa Mungu, ili nguvu ya Kristo mfufuka iweze kuyashinda yote.
Baba Mtakatifu
Francisko katika tafakari hii, mbele ya Sanda Takatifu, anapenda kusali kwa kutumia
maneno ya Mtakatifu Francisiko wa Assisi aliyosali mbele ya Msalaba akimwomba Mwenyezi
Mungu aweze kuliangazia giza la moyo wake, amkirimie imani thabiti, matumaini na mapendo
ya kweli; aweze kuwa na upeo wa kuelewa ili hatimaye, aweze kutekeleza kwa dhati kabisa
ile amri ya upendo.