Sanda Takatifu inaonesha imani na nguvu ya upendo wa Mungu kwa binadamu
Askofu mkuu Cesare Nosiglia wa Jimbo kuu la Torino, Italia katika ujumbe wake kwa
Siku kuu ya Pasaka kwa Mwaka 2013, anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema,
kumwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa sifa na shukrani kwa kulijalia Kanisa kumpata Mchungaji
Mkuu, Baba Mtakatifu Francisko, anayechomoza kama miali ya jua la alfajiri.
Papa
amepokelewa na waamini pamoja na watu wenye mapenzi mema kwa mikonomiwili, alama ya
Pasaka Mpya katika Kanisa, inayotolewa na Kristo mwenyewe kwa kulipatia Kanisa lake
na ulimwengu kwa ujumla, nguvu na ujasiri wenye matumaini. Huu ni mwaliko na changamoto
ya kutolea ushuhuda wa imani tendaji, kwa kupokea na kukumbatia Msalaba unaokoa; chemchemi
ya wokovu na upendo wa Mungu, unaopaswa kupelekwa kwa maskini na wanyonge ndani ya
Jamii.
Waamini wanahamasishwa kulinda na kutunza mazingira; kujenga na kuimarisha
umoja, udugu na mshikamano wa dhati kwa kuondokana na kinzani na vikwazo vinavyopelekea
migawanyiko katika Jamii. Baba Mtakatifu Francisko, tangu kuchaguliwa kwake, ameonesha
kuwa ni mtu wa watu na kwa ajili ya watu, ili kuweza kuwaonesha ile njia inayokwenda
kwa Kristo.
Ameonesha na kushuhudia kwa njia ya maisha na utume wake, maana
ya uongozi kuwa ni kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kuwahudumia wanyonge na
maskini. Kwa muda mfupi, Baba Mtakatifu Francisko ameendelea kuwashirikisha ndugu
zake katika Kristo fadhila na utajiri wake wa imani na mapungufu yake ya kibinadamu.
Mwaka
huu, wakati wa Jumamosi kuu, Sanda Takatifu imeoneshwa kwa njia ya Luninga, kutoka
katika Kanisa kuu la Jimbo kuu la Torino, tukio ambalo waamini na watu wenye mapenzi
mema wamelifuatilia kwa unyenyekevu mkubwa kwa kuona ile nguvu ya upendo wa Mungu
unaojionesha kwa njia ya Sadaka ya Yesu Kristo pale Msalabani.
Ndani ya Kanisa
kuna watu wanaobeba Misalaba ya maisha, alama makini ya mateso ya Kristo, changamoto
kwa waamini hawa kuuishi Msalaba wao kwa Imani, wakijitahidi kutekeleza mapenzi ya
Mungu katika maisha yao, daima wakiwa tayari kujitoa sadaka kwa ajili ya jirani zao!
Sanda
Takatifu inaonesha kwamba, kupenda maana yake ni kuteseka na kujitoa bila ya kujibakiza
kwa ajili ya Kristo, Kanisa na mafao ya wengi, kwa kutambua kwamba, upendo wa Mungu
unashinda maovu ya dunia hii na kwamba, mema yanaweza kuleta mabadiliko ya pekee katika
maisha ya mwanadamu kuelekea katika safari ya ukombozi.
Sanda Takatifu inayooneshwa
Jumamosi Kuu inamwonesha Kristo Msulubiwa, Imani na nguvu ya Upendo wa Mungu unaomwezesha
mwanadamu kufufuka kutoka katika wafu; kuonja matumaini ya ushindi wa Mungu dhidi
ya dhambi na mauti kwa njia ya Yesu Kristo Mfufuka. Ni changamoto kwa waamini kukumbatia
msamaha dhidi ya chuki na uhasama na kuendelea kujikita zaidi katika maisha, sala
na upendo, kiasi hata cha kuonesha upendo huu katika wito wa maisha ya Kipadre, Kitawa
na Ndoa Takatifu.
Ni changamoto ya kusimama kidete kulinda na kudumisha haki
msingi za binadamu, utu na heshima ya binadamu; kutafuta kwanza kabisa mafao ya wengi;
daima haki, amani, upendo na mshikamano vikipewa msukumo wa pekee. Kila mtu aliyeumbwa
kwa sura na mfano wa Mungu anapaswa kupokelewa, kuthaminiwa na kupendwa bila kubezwa
wala kutezwa kutokana na hali yake ya maisha; kama kilema, mgonjwa, mhamiaji au mtu
aliyesukumizwa pembezoni mwa Jamii. Kipindi cha Pasaka kiwe ni kielelezo cha ushuhuda
wa imani tendaji, kila mwamini ajitahidi kuwa chembe chembe ya matumaini katika ulimwengu
mamboleo.