2013-03-30 08:04:27

Salam za kheri na matashi mema kwa Papa Francisko kwa Siku kuu ya Pasaka 2013


Rais Giorgio Napolitano wa Italia amemwandikia salam za kheri na baraka Baba Mtakatifu Francisko wakati huu anapoadhimisha Siku kuu ya Pasaka kwa mara ya kwanza kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Kwa niaba yake mwenyewe na wananchi wa Italia katika ujumla wao, anachukua fursa hii kumtakia Baba Mtakatifu Francisko mafanikio mema katika maisha na utume wake.

Rais Napolitano anasema, Maadhimisho ya Siku kuu ya Pasaka kwa Mwaka huu yanafanyika wakati nchi ya Italia ikiwa inakabiliana na changamoto kubwa za mabadiliko katika mfumo wake wa demokrasia na uongozi wa ngazi za juu katika mihimili mikuu ya uongozi kitaifa.

Hii ni changamoto ya kujenga utamaduni wa kusikiliza na kutoa kipaumbele cha kwanza katika masuala ya amani, haki na mshikamano pamoja na kutafuta nguvu inayohitajika ili kuweza kupokea ujumbe wa Kikristo na ule wa jumla unaopania kuwa ni mwanzo mpya sanjari na kuwajengea watu matumaini mapya yanayoendelea kujionesha sehemu mbali mbali za dunia.

Rais Giorgio Napolitano anahitimisha salam na ujumbe wa matashi mema ya Pasaka kwa Baba Mtakatifu Francisko, huku akimwahakikishia urafiki na ushirikiano anapotekeleza utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.







All the contents on this site are copyrighted ©.