MSALABA ni kielelezo cha: Upendo, huruma, msamaha na hukumu!
Baba Mtakatifu Francisko kwa mara ya kwanza, tangu alipochaguliwa kuwa Khalifa wa
Mtakatifu Petro, ameshiriki katika Ibada ya Njia ya Msalaba, iliyofanyika kuzunguka
magofu ya Colosseo yaliyoko mjini Roma, Ijumaa kuu, tarehe 29 Machi 2013, Usiku, ibada
ambayo imehudhuriwa na umati mkubwa wa watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia.
Mara
baada ya ibada ya Njia ya Msalaba, Baba Mtakatifu Francisko amewashukuru wale wote
waliohudhuria Ibada hii sanjari na wote waliokuwa wanaifuatilia kwa njia za mwasiliano
ya Jamii. Kwa namna ya pekee, amewakumbuka wagonjwa na wazee, wanaoendelea kuibeba
Misalaba katika hija ya maisha yao ya kila siku. Baba Mtakatifu anasema, MSALABA unapaswa
kuwa ndiyo neno msingi katika maadhimisho ya Njia ya Msalaba.
Msalaba ni jibu
makini ambalo Mwenyezi Mungu kwa njia ya Mwanaye Mpendwa Yesu Kristo amelitoa kwa
walimwengu dhidi ya dhambi. Wakati mwingine Mwenyezi Mungu anaamua kukaa kimya, lakini
hata katika ukimya huu, bado anaendelea kuzungumza na kujibu kilio cha waja wake kwa
njia ya Fumbo la Msalaba.
Baba Mtakatifu anasema Msalaba unafumbata kwa namna
ya pekee: upendo, huruma, msamaha na hukumu. Mwenyezi Mungu anamhukumu mwanadamu kwa
kumwonjesha upendo, ikiwa kama mwanadamu ataweza kulipokea pendo hili, atapata uzima
wa milele, lakini akilitema, kwa hakika atakuwa amejihukumu mwenyewe, kwani kimsingi
Mwenyezi Mungu anapenda na kuokoa.
Baba Mtakatifu anakumbusha kwamba, Msalaba
ni jibu makini kwa Wakristo dhidi ya magumu yanayowaandama na kuwazunguka katika hija
ya maisha na utume wao, changamoto kwa waamini kujibu ubaya kwa kutenda wema, kwa
kujitwika Msalaba kama alivyofanya Kristo mwenyewe. Itakumbukwa kwamba, Taafakari
ya Njia ya Msalaba na Sala kuzunguka Magofu ya Colosseo kwa Mwaka 2013 imetayarishwa
na vijana wawili kutoka Lebanon na kuhaririwa na Kardinali Butros Becharà Rai, Patriaki
wa Kanisa la Wamaroniti wa Lebanoni.
Baba Mtakatifu Francisko ametumia fursa
hii kuwashukuru wote waliohusika kwa ushuhuda huu makini, kumbu kumbu endelevu ya
hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita nchini Lebanon.
Tafakari hii imeonesha na kugusa ile nguvu ya ushuhuda wa umoja wa Wakristo katika
Nchi Takatifu; urafiki na udugu miongoni mwa Wakristo, Waislam na Waamini wa dini
nyingine. Tukio hili ni kielelezo cha matumaini mapya kwa Nchi za Mashariki ya Kati
na Ulimwengu kwa ujumla.
Baba Mtakatifu Francisko mwishoni, anawaalika waamini
kuendeleza Njia ya Msalaba katika maisha ya kila siku. Anawaalika kutembea katika
Njia ya Msalaba, wakibeba ndani mwao upendo na msamaha; wakiwa na matumaini katika
ufufuko wa Kristo, aliyewapenda upeo na kwamba, kila kitu ni upendo!
Umati
mkubwa wa watu ulizunguka magofu ya Colosseo, wakati ambapo Kardinali Agostino Vallini,
Makamu Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Roma alipokuwa anaongoza Ibada ya Njia ya Msalaba,
iliyokuwa na uwakilishi mzito kutoka: Lebanon, Italia, India, China, Nchi Takatifu,
Afrika na Brazil. Mara baada ya Ibada ya Njia ya Msalaba, Kwaya ya Makleri kutoka
Lebanon, iliimba. Kwa hakika, tafakari na sala ya Njia ya Msalaba kwa Mwaka 2013 ilikuwa
na ujumbe mzito!