2013-03-30 10:02:43

Kukamatwa kwa mtuhumiwa wa mauaji ya Padre Evaristi Mushi, Jimboni Zanzibar uwe ni mwanzo wa kufahamu nani anahusika na chokochoko za kidini Tanzania!


Maafisa wa Upepelezi wa Jeshi la Polisi Tanzania kwa kushirikiana na na Makachero wa Shirika la Upelelezi la Marekani, FBI, kwa pamoja wamefanikiwa kumtia pingu Omar Mussa Makame (35) anayetuhumiwa kumuua kwa kumpiga risasi Padre Evarist Mushi wa Jimbo Katoliki Zanzibar, kunako tarehe 17 Februari 2013.

Hayo yamebainishwa na Kamishina wa Jeshi la Polisi Zanzibar, Mussa Alli Mussa na kwamba, hatua zaidi za kisheria zimekwishachukuliwa na mtuhumiwa anatarajiwa kufikishwa Mahakamani mapema iwezekanavyo.

Wachunguzi wa masuala ya haki msingi za binadamu, utawala wa sheria na uhuru wa kuabudu wanasema, hii ni hatua ya kwanza katika mchakato wa kuhakikisha kwamba, sheria inashika mkondo wake. Lakini jambo la msingi ambalo watanzania kwa sasa wanataka kulifahamu ni nani anayehusika na choko choko za kidini ambazo kwa sasa zimewajengea watanzania wengi hofu hata ya kuanza kuogopa kwenda Makanisani kusali?

Changamoto kwa wakati huu ni kuendeleza majadiliano ya kidini ili haki, amani, umoja na mshikamano wa kitaifa viweze kutawala tena na kamwe watanzania wasikubali kutumiwa na baadhi ya watu wanaotaka kuvuruga amani, upendo na mshikamano wa kitaifa kwa mafao yao wenyewe!







All the contents on this site are copyrighted ©.