2013-03-30 10:28:03

Jumuiya ya Kimataifa yashindwa kufikia muafaka kuhusu udhibiti wa biashara ya silaha duniani!


Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon ameonesha masikitiko yake makubwa baada ya wajumbe wa mkutano wa Umoja wa Mataifa uliokuwa unajadili kuhusu mkataba wa biashara ya siilaha kimataifa kuhitimishwa mwishoni mwa juma, bila kufikia muafaka.

Wajumbe kutoka Korea ya Kaskazini, Iran na Syria, baada ya majadiliano kwa takribani majuma mawili waliamua kupinga mkataba huu na hivyo Jumuiya ya Kimataifa ikajikuta inakwama katika utekelezaji wake.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anabainisha kwamba, Mkataba huu ni muhimu sana na umeandikwa kwa ufasaha kwa kuangalia mahitaji ya Jumuiya ya Kimataifa kwa wakati huu. Ni matumaini ya Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa kwamba, Nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa, watajipanga kwa mara nyingine, ili kuweza kuupitisha Mkataba huu kwa kupigiwa kura na wajumbe wapatao theluthi mbili.

Wajumbe wengi walianza kuonesha matumaini ya Mkataba huu kuweza kupitishwa na hivyo kuwa ni tukio la kihistoria, baada ya Rais Barack Obama wa Marekani kutoa changamoto kubwa katika udhibiti wa silaha nchini Marekani. Wachunguzi wa mambo wanasema kwamba, waathirika wakuu wa biashara ya silaha kimataifa ni watu wanaoishi Barani Afrika na Amerika ya Kusini.

Wakati wa ufunguzi wa mkutano huu hapo tarehe 18 Machi 2013, Wajumbe kutoka Barani Afrika walikuwa wameitaka Jumuiya ya Kimataifa kuweka viwango vya hali ya juu kimataifa, ili kukomesha biashara haramu ya silaha kimataifa, ambayo imekuwa ni chanzo cha vita, kinzani na vurugu za kijamii Barani Afrika na sehemu nyingine za dunia.

Akichangia mada katika mkutano huu, Rais Ellen Jonhson Sirleaf wa Liberia ambaye pia ni mshindi wa tuzo la amani, amesema kwamba, kuna mamillioni ya watu wanaendelea kupoteza maisha na wengine wengi kupata majeraha na ulemavu wa kudumu kutokana na kuzagaa kwa silaha za moto!







All the contents on this site are copyrighted ©.