2013-03-29 07:27:32

Njia ya Msalaba: daraja linalowavusha watu kutoka katika mauti ili kupata maisha mapya!


Tafakari ya Njia ya Msalaba kuzunguka Magofu ya Colosseo iliyoandaliwa na Vijana kutoka Lebanon na kuhaririwa na Kardinali Bèchara Boutros Rai, Patriaki wa Kanisa la Maroniti la Antiokia. RealAudioMP3
Ni mwaliko kwa wafuasi wa Kristo kutumia Msalaba kama daraja linalomvusha mwanadamu kutoka katika kifo kuelekea maisha ya uzima wa milele. Ni changamoto kwa vijana na wote wanaokumbana na kinzani, migogoro na migawanyiko ya kikabila, kidini na kijamii; wanaokabiliana na vita na ukosefu wa haki msingi; vijana wanatakiwa na Mama Kanisa kuwa ni alama ya matumaini na wajenzi wa amani.
Hata leo hii mchakato wa kumhukumu Yesu bado unaendelea kutokana na ukweli kwamba, kuna baadhi ya watu wanapenda kumng’oa Mungu kutoka katika maisha na vipaumbele vya mwanadamu. Kuna baadhi ya watu wanaotaka kufisha tunu za imani, utu na maadili mema kwa kisingizio cha kutaka kulinda na kudumisha demokrasia na uhuru wa kuabudu. Watu wanaoteseka na kudhulumiwa hasa walioko Mashariki ya Kati wauone Msalaba kama alama ya matumaini, ili hatimaye, waweze kuona ukweli na kuonja upendo.
Yesu bado anawaalika waamini kusimama na kuendelea mbele na hija ya maisha yao ya kiroho hata baada ya kuanguka, kusimama na kuendelea na safari ya kuutafuta ukweli kwa kutumia vyema imani na akili yake, ili kweli aweze kupata utimilifu wa ukweli wote.
Bikira Maria Mama wa Mungu na Kanisa ni mfano bora wa kuigwa. Ni Tabernakulo ya kwanza ya Neno la Mungu; ni mwanfunzi makini aliyejifunza kufanya tafakari ya kina katika ukimya, akabahatika kukutana naye katika Njia ya Msalaba. Hata leo hii, bado wazazi wengi wanaendelea kuteseka kutokana na mateso ambayo wazazi wanawapatia watoto wao au watoto wanawafanyia wazazi wao. Hii ni changamoto ya kuhakikisha kwamba, Familia za Kikristo zinakuwa ni mahali muafaka pa kukutana na kuonesha uwapo endelevu wa Yesu katika hija ya maisha ya watu wake; daima wakijitahidi kuiga mfano wa Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu.
Kila mtu ana Msalaba wake, lakini katika yote haya, waamini wanapaswa kujifunza kukubali na kuipokea Misalaba ya maisha yao kwa imani, mapendo na matumaini; wakiendelea kuwa na dhamiri hai, wakisikiliza kwa makini, wakiwa na kiu ya kutaka kufahamu ukweli pamoja na kutumia vyema uhuru wao wa kuabudu.
Waamini katika hija ya maisha yao hapa duniani wanautafuta Uso wa Yesu, changamoto kwa waamini na watu wenye mapenzi mema kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu, utu na heshima ya wote, hasa wale wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kutokana na umaskini, ujinga na maradhi.
Yesu anapoanguka mara ya pili, anawachangamotisha waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kuangalia kinzani na migogoro ya kidini inayoendelea kufuka moshi sehemu mbali mbali za dunia, ili kwa kuwa na dhamiri nyofu, waoneshe utashi wa majadiliano ya kidini na ushirikiano wa dhati licha ya tofauti zao za kiimani. Kwa pamoja wasimame kidete kulinda na kutetea uhuru wa kuabudu, maendeleo, mafao na ustawi wa wote. Katika mahangaiko yote haya, waamini wanaalikwa kutolea ushuhuda wa imani na upendo wa Kristo kwa wote.
Waamini wanakumbushwa kwamba, dunia ya leo imesheheni wanawake wanaodhulumiwa na kunyanyaswa utu na heshima yao, wanaobaguliwa na kutengwa. Wote hawa Kristo awe ni amani yao. Bikira Maria aliyebahatika kuwa ni Tabernakulo ya Fumbo la Umwilisho, ameuinua utu na heshima ya kila mwanamke. Yesu awe kweli ni faraja ya wanawake wanaoteseka sehemu mbali mbali za dunia.
Yesu anapoanguka mara ya tatu, anawakumbusha waamini kwamba, uzito wa dhambi za binadamu unamwelemea. Anamwonesha binadamu kwamba, hata katika udhaifu wake bado anaweza kushinda magumu na vishawishi akaamka na kusonga mbele, kwa kuchota neema na baraka kutoka katika Sakramenti za Kanisa; ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa; Umoja na Mshikamano wa dhati; upendo na unyenyekevu. Msalaba wa Kristo uwe ni daraja linalowaunganisha waamini kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa.
Kuna watu sehemu mbali mbali za dunia wanaendelea kuvuliwa utu na heshima yao kutokana na madhulumu kiasi cha kukimbia hata makazi yao wenyewe. Wote hawa wawe na ujasiri wa kubaki katika maeneo yao, ili kuendelea kutangaza Habari Njema ya Wokovu, kwa kutambua kwamba, Mwenyezi Mungu daima yuko kati yao!
Yesu aliyefungwa mikono na miguu pale Msalabani kwa njia ya misumari aendelee kuwaombea binadamu wote, ili kwa jicho lake la upendo kutoka pale Msalabani, aweze kuwaponya wagonjwa na kuwasamehe wadhambi na upendo wake uweze kuifunika dunia yote. Kanisa linawaombea vijana wanaokata tamaa kiasi cha kujikuta wakitumbukia katika matumizi haramu ya dawa za kulevya; wakijiingiza katika madhehebu na anasa, ili waonje upendo na kupata furaha ya kweli kutoka kwa Kristo.
Yesu anapokufa pale Msalabani, Kanisa linayaelekeza macho yake kwa wale wote wanaokumbatia utamaduni wa kifo, kutubu na kuongoka, ili waweze kuuona ukweli na wajenzi wa utamaduni wa upendo na watangazaji hodari wa Injili ya Uhai.
Yesu anapozikwa Kaburini, hapo baadhi ya watu wanadhani kwamba, ubaya na dhambi vimeshinda na kwamba: sauti ya ukweli, upendo, haki na amani haina nafasi tena. Vitendo vya kigaidi, mauaji, chuki na hali ya kulipizana kisasi vinaonekana kushamiri.
Kanisa linachukua nafasi hii kwa ajili ya kuwaombea waathirika wa vitendo vya kigaidi sehemu mbali mbali za dunia, wakimbizi na watu wasiokuwa na makazi waweze kurejea tena katika makazi yao; damu ya watu wasiokuwa na hatia inayoendelea kumwagika iwe ni mbegu ya kuimarisha umoja, upendo na mshikamano wa kidugu, ili dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi, kwa kukazia na kudumisha tunu msingi za kitamaduni, maisha ya kiroho na kiutu.
Mbele ya kifo, mateso na machungu ya maisha, hapa kunahitajika matumaini nai mani thabiti. Mateso, kifo na ufufuko wa Yesu ni changamoto ya kutembea katika mwanga wa maisha mapya, kwa kuonesha umuhimu wa zawadi ya maisha, kwa wale wote waliokata tamaa ya maisha, kwani Kanisa lina amini katika ushindi wa Kristo dhidi ya dhambi na mauti.







All the contents on this site are copyrighted ©.