Nimewapeni mfano, nanyi hudumianeni kwa ukarimu na upendo!
Baba Mtakatifu Francisko, Jioni ya Alhamisi kuu, tarehe 28 Machi 2013 ameadhimisha
Ibada ya Karamu ya Mwisho, katika Gereza la Watoto la "Casal del Marmo," lililoko
mjini Roma kwa kuwaosha miguu watoto kumi na wawili, kielelezo cha upendo wa Kristo
unaomwilishwa katika huduma kwa jirani, lakini zaidi kwa wale wanaosukumizwa pembezoni
mwa Jamii.
Katika mahubiri yake kwa vijana hawa, amewashirikisha upendo ulioneshwa
na Yesu Kristo, Siku ya Alhamisi kuu, alipoweka mavazi yake kando, akaanza kuwaosha
mitume wake miguu, kitendo ambacho kilimshangaza Mtume Petro, kiasi cha kutaka kukataa
katu katu kuoshwa miguu na Yesu, lakini akafafanuliwa maana yake, kiasi kwamba, akaweza
hata kuridhika na uamuzi uliotolewa.
Yesu ambaye ni Mwalimu na Bwana, Nafsi
ya Pili ya Fumbo la Utatu Mtakatifu, ndiye aliyetekeleza kitendo hiki cha unyenyekevu,
ambacho kilikuwa kinafanywa na watumwa! Akawaachia mfano wa kuigwa na kuendelezwa,
kwa kutambua kwamba, uongozi ni huduma hasa kwa wanyonge na wale wanaosukumizwa pembezoni
mwa Jamii.
Ni mwaliko wa kumegeana upendo unaobubujika kutoka kwa Kristo,
aliyewapenda watu wake upeo kiasi cha kuyamimina maisha yake pale juu Msalabani. Huduma
ya upendo, iwachangamotishe waamini na watu wenye mapenzi mema kujikita katika msamaha
na upatanisho unaopaswa kububujika kutoka katika undani wa mtu mwenyewe.
Baba
Mtakatifu Francisko anasema, kama Padre na Askofu wa Roma, anajisikia kuwajibika kuwaonjesha
huruma na upendo wa Kristo kwa njia ya huduma inayopata chimbuko lake kutoka katika
moyo wake na wala si jambo la kutaka kujionesha mbele ya watu.
Kwa maneno
machache, hii ni imani katika matendo, inayowachangamotisha waamini na watu wenye
mapenzi mema, kusaidiana kwa hali na mali; wakiungana kwa pamoja kutafuta mafao ya
wengi. Huduma ya upendo ni changamoto endelevu inayotolewa na Yesu aliyekuja kutumikia
na kuyamimina maisha yake kwa ajili ya ukombozi wa wengi.