2013-03-29 08:02:21

Imani ya Kanisa imesimikwa katika Yesu Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka!


Baba Mtakatifu Francisko katika utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, anaendelea kuwahamasisha waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema, kujikita katika mchakato wa majadiliano ya kidini na kiekumene, ili kuweza kulinda na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo, udugu na upatanisho wa kweli, kama alivyofanya Mtakatifu Francisko wa Assisi enzi ya uhai wake. RealAudioMP3

Alipinga vita vya kidini na kutaka waamini kujenga utamaduni wa upatanisho kama njia ya kuimarisha amani na uelewano kati ya watu wa dini mbali mbali na kwamba, tofauti zao za kiimani, kisiwe ni kisingizio cha kuleta vita na machafuko miongoni mwa Jamii.

Kardinali Polycarp Pengo, Rais wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar ambaye pia ni Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, katika mahojiano na Radio Vatican anabainisha kwamba, Kanisa linamwamini Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu, changamoto ya kudumisha misingi ya haki, amani na upatanisho wa kweli, kwani kwa njia ya Damu yake Azizi, ameukomboa ulimwengu na kumpatanisha mwanadamu na Muumba wake.

Jumuiya ya Kimataifa inapaswa kujifunza kwamba, sera ya vita na matumizi ya nguvu zimepitwa na wakati na matokeo yake ni watu wasiokuwa na hatia kuendelea kupoteza maisha yao, badala yake, Jumuiya ya Kimataifa inapaswa kujikita katika majadiliano ya kina, ili haki, amani na upatanisho viweze kustawi na kushamiri tena miongoni mwa Jamii.

Kardinali Pengo katika mahojiano na Radio Vatican amegusia pia chokochoko za kidini zinazoendelea kushika kasi nchini Tanzania. Wito wake ambao ameendelea kukazia wakati wote ni kuwataka Wakristo na watanzania wenye mapenzi mema, kujikita katika mchakato wa kutafuta misingi ya haki na amani kwa njia ya majadiliano ya kina yanayosimikwa katika ukweli, uwazi na upendo miongoni mwa Jamii, daima wote wakipania kutafuta: ustawi, mafao na maendeleo ya wengi, kwani amani ni jina jingine la maendeleo.

Kardinali Pengo anawakumbusha Wakristo kwamba, wanamfuata Kiongozi wao ambaye ni Yesu Kristo, aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu ili kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti. Kwa njia hii akawashirikisha wafuasi wake katika ujenzi wa Ufalme wa Mungu unaosimikwa katika amani. Hiki ni kielelezo kwamba, Kristo anawatakia amani wafuasi wake; amani ambayo wanapaswa pia kuwashirikisha wengine katika hija ya maisha yao!

Kuchukua silaha na kuanza mapambano ni kinyume cha mafundisho ya Kristo na kamwe Wakristo wajishikwe na kishawishi cha kutaka kulipiza kisasi, kwani Yesu Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka ili kumkirimia mwanadamu amani ya kweli. Ni changamoto ya kukoleza mchakato wa majadiliano ya kidini; kwa kuheshimiana na kuthaminiana kama watu walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.







All the contents on this site are copyrighted ©.