Vijana wajibikeni kikamilifu katika maisha ya kiraia, kijamii na kiroho!
Askofu Gevas Nyaisonga wa Jimbo Katoliki Dodoma, Tanzania katika Maadhimisho ya Jumapili
ya Matawi sanjari na Siku ya Vijana Kijimbo, amewataka vijana nchini Tanzania kuwajibika
kikamilifu katika maisha ya Kijamii na Kiroho kwa ajili ya ustawi na maendeleo yao
kama vijana, lakini zaidi kama watanzania.
Juma kuu ni
kipindi maalum kinachotoa fursa kwa waamini kufanya tafakari ya kina kuhusu Mafumbo
ya Ukombozi, yaani mateso, kifo na ufufuko wa Kristo.
Askofu Nyaisonga anabainisha
kwamba, tangu awali, vijana wamekuwa na mchango wa pekee kabisa katika historia ya
ukombozi wa mwanadamu. Siku ya Vijana Kijimbo kwa mwaka huu imekwenda sanjari na Maadhimisho
ya Mwaka wa Imani, changamoto kwa vijana kuifahamu, kuiadhimisha, kuimwilisha katika
matendo adili na kuisali. Nchini Tanzania, mchakato wa kuandika Katiba Mpya inayotarajiwa
kutumika katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 unaendelea. Hii ni sheria mama.
Askofu
Nyaisonga amewakumbusha vijana kwamba, Katiba nzuri ni ile iliyoandikwa na kuridhiwa
na wananchi wenyewe, ili iweze kuwa ni dira na mwongozo katika maisha yao, daima wakiwa
tayari kuilinda na kuitetea kwa udi na uvumba. Baada ya kuchangia maoni yao, sasa
wanahamasishwa kujitokeza kujiunga katika Mabaraza ya Katiba, ili kuchangia katika
maboresho ya Katiba itakayokuwa ni mhimili mkuu wa sheria za nchi.
Utakapofika
wakati wa kupiga kura ya maoni kuhusu muswada wa Katiba Mpya, wananchi na hasa vijana
wanapaswa kujitokeza kwa wingi. Hii inatokana na ukweli kwamba, vijana wengi hawapendi
kujishughulisha na masuala yanayowahusu wakidhani kwamba, hayo ni mambo ya wazee,
lakini huu ni wajibu wao wa kiraia na kijamii wanaopaswa kuutekeleza kwa umakini mkubwa.
Askofu
Nyaisonga amewataka vijana ambao kwa sasa wanaunda kundi kubwa la wasomi wa Tanzania
kujitokeza kuchangia katika mijadala ya Muswada wa Katiba, wakiongozwa na vipaumbele
vya kitaifa yaani: mafao ya wengi, utu na heshima ya binadamu; umoja, upendo, udugu
na mshikamano wa kitaifa. Wasimame kidete kulinda na kutetea uhuru wa kidini na kamwe
wasikumbatie udini unaoweza kujitokeza katika Muswada wa Katiba, hata ikiwa ni kwa
ajili ya dini yao, kwani hapa kuna hatari kubwa ya kuligawa taifa kwa misingi ya udini,
ukabila na mahali anapotoka mtu.
Ikiwa kama mambo haya msingi hayataonekana
katika Muswada wa Katiba Mpya, vijana wanahaki yakupaaza sauti yao kuuliza, kulikoni?
Na kwa hakika watasikilizwa kwani hii ni haki yao msingi, wakinyama ni kuridhia mambo
ambayo yatakuwa ni hatari kwa siku za usoni.
Askofu Gervasi Nyaisonga wa Jimbo
Katoliki Dodoma, ametumia fursa ya Maadhimisho ya Siku ya Vijana Kijimbo kupembua
wajibu wa vijana katika maisha ya kijamii. Anasema, kuna wakati nchini Tanzania kulivuma
mauaji ya vikongwe kutokana na imani za kishirikina, watu wengi wakaa kimya wakidhani
kwamba, jambo hili lilikuwa haliwagusi, lakini hofu na mashaka yakaendelea kujengeka
miongoni mwa watanzania hasa miongoni mwa wazee.
Kukaibuka mauaji ya watu
wenye ulemavu wa ngozi, baadhi ya watu wakadhani kwamba ni tatizo lililokuwa linawagusa
watu wenye uchu wa mali na madaraka kwa kukumbatia imani za kishrikina, watanzania
wengi wakaendelea kuyapuuzia matukio haya, kwa vile tu, hayakuwagusa moja kwa moja!
Katika miaka ya hivi karibuni, kukaibuka tena wimbi la mashambulizi na uharibifu
wa Nyumba za Ibada na mali za Serikali na watu wa binafsi. Baadhi ya watu wakaanzisha
mtindo wa kuchoma mali za watu! Watanzania wakaendelea kukaa kimya kana kwamba, hakuna
jambo lililokuwa linatendeka! Kukaibuka malumbano na kashfa za kidini na hatimaye,
dhuluma na mauaji ya viongozi wa kidini. Watanzania wakasema, haya ni matukio yanayotendwa
na wahuni wachache! Lakini Askofu Nyaisonga anasema, kwamba, matukio yote haya yanafunja
umoja, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa, ambao Tanzania imekuwa ikijivunia kwa
takrbani miaka 50 iliyopita.
Mambo hayakuishia hapa, kuna mwakilishi wa madaktari
wakati wakidai haki zao, alikamatwa na kupigwa; hivi karibuni, mwandishi wa habari
alikung’utwa kisawa sawa, hadi kupelekwa nje kwa matibabu ya dharura! Haya ni matukio
yanayogusa taaluma na kimsingi wahusika wakuu ni vijana. Askofu Nyaisonga amewaonya
vijana kutojiingiza katika masuala yanayopelekea uvunjifu wa misingi ya haki, amani,
utulivu na mshikamano wa kitaifa, bali wasimame kidete kulinda, kutetea na kutangaza
Injili ya Upendo na Mshikamano kati ya watu!
Askofu Nyaiosonga katika Maadhimisho
ya Siku ya Vijana Kijimbo yaliyohudhuriwa na umati mkubwa wa vijana kutoka Jimboni
Dodoma, aligusia pia umuhimu na wajibu wa vijana katika maisha ya kiroho, kwa kuwataka
kukuza moyo wa sala, ibada na tafakari ya Neno la Mungu. Amewakumbusha vijana kusali
daima ili wasije wakatumbukia katika kishawishi, lakini jambo la kushangaza ni kuona
kwamba, vijana engi wanafurahia kutumbukia au kutumbukizwa katika majaribu, lakini
daima wakumbuke kwamba, sala ni mkombozi wao!
Askofu Nyaisonga anaendelea kusema
kwamba, vijana wengi wamekosa fadhila ya utii kwa wazazi, walezi na wakuu wao wakidhani
kwamba, utii kwa sasa umepitwa na wakati, lakini utii ni fadhila muhimu sana katika
maisha ya kijamii. Amekumbusha kwamba, haki inakwenda sanjari na wajibu. Kumezuka
mtindo nchini Tanzania kwa baadhi ya watu kudai haki zao, kiasi hata cha kukiuka haki
msingi za binadamu. Kuna baadhi ya vijana wanataka kujipatia sifa, lakini kwa bahati
mbaya wanajikuta wakiwa wameponzwa, kwani sifa njema zinarandana na dira ya maisha
ya mtu!
Askofu Nyaisonga amewataka vijana kamwe wasikate tama na maisha, matokeo
yake ni kukengeuka na kupoteza dira na mwelekeo wa maisha, kiasi cha kujitumbukiza
katika vitendo vya ovyo! Vijana waongozwe na dhamiri nyofu, wawe na msimamo wa maisha
na kamwe wasifuate upepo wa makundi ya vijana wenzao. Kila jambo walipime kwa umakini
na busara kubwa na kamwe wasitafute njia ya mkato katika maisha, hii itawaponza! Kuna
vijana wenye tamaa ya kupata maendeleo kwa haraka, lakini matokeo yake wanajikuta
wakizama katika mambo ya ovyoooo!
Huu ni wakati wa maendeleo ya sayansi na
teknolojia. Askofu Nyaisonga anasema, kuna baadhi ya vijana wamejikuta wakiwa ni watumwa
wa maendeleo ya sayansi na teknolojia: ni watumwa wa Computer na simu za viganjani,
ni watu waliobobea katika mawasiliano yasiyo na tija! Baadhi yao wanajiamini mno kupita
kiasi; hawashauriki wala kuonyeka!
Askofu Gervas Nyaisonga wa Jimbo Katoliki
Dodoma ameyatumia Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kutoa Katekesi ya kina na
dira makini kwa vijana, akitambua kwamba, wao ndio jeuri na nguvu ya mabadiliko hasi
na chanya ndani ya Jamii. Wanawajibika kushiriki kikamilifu katika majukumu yao kijamii
na kiroho!