Papa bado ataendelea kuishi kwa muda Domus Sanctae Marthae
Baba Mtakatifu Francisko ameonesha utashi wa kuendelea kuishi kwa muda katika makazi
yake ya muda yaliyoko Domus Sanctae Marthae. Hayo yamebainishwa na Padre Federico
Lombardi, Msemaji mkuu wa Vatican, baada ya Baba Mtakatifu Francisko kuadhimisha Ibada
ya Misa Takatifu kwenye Kikanisa kilichoko kwenye makazi haya ya muda, siku ya Jumanne,
tarehe 26 Machi 2013.
Kwa sasa Baba Mtakatifu amehama kutoka kwenye chumba
alichokuwa anakitumia wakati wa Conclave na kwa sasa amepewa chumba kikubwa zaidi,
kinachomwezesha walau kukutana na kuzungumza na watu mbali mbali wanaomtembelea kwa
wakati huu.
Padre Lombardi anafafanua kwamba, shughuli zake za kichungaji,
mikutano ya kiofisi na makundi ya watu anatumia Ofisi za Kipapa zilizoko kwenye Jengo
la Kipapa. Hapa kuna Ukumbi wa Clementina unaotumiwa wakati wa mikutano na makundi
makubwa ya watu, kuna Maktaba binafsi na mazingira maalum kwa ajili ya utume na maisha
ya Khalifa wa Mtakatifu Petro. Lakini kwa makazi na Ibada ya Misa Takatifu anarudi
kwenye Hosteli ya Mtakatifu Martha.