2013-03-27 10:50:44

Jitahidini kuwa Wakristo na Wakatoliki kweli kweli kwa maneno na matendo yenu!


Askofu msaidizi Lorenzo Leuzzi wa Jimbo kuu la Roma, anasema, alipoteuliwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kuwa Askofu msaidizi wa Jimbo kuu la Roma, mawazo yake yaliruka moja kwa moja hadi kwa Mtakatifu Monica, ambaye katika maisha alitamani kumwona Mwanaye mpendwa Augustino aliyekuwa ametopea katika malimwengu akiwa Mkristo na Mkatoliki kweli kweli; katika maneno na matendo yake.
Hakuwa na jambo jingine ambalo alilitamani katika ulimwengu huu ambao kwake ulisheheni magumu na majonzi tupu! Mama Monica alifurahi sana aliposikia kwamba, Mwanaye Augostino ameongoka na baadaye ameteuliwa kuwa Askofu. Hii ni furaha kubwa iliyokuwa inavuka matumaini na matarajio yake.
Askofu msaidizi Leuzzi anasema hiki ni kielelezo makini cha matamanio ya Mama mwenye imani na matumaini thabiti, tunu ambazo kwake amezipokea na kama kielelezo kikubwa cha zawadi ya imani katika hija ya maisha yake. Pengine kwa walimwengu jambo hili linaweza kuonekana kuwa ni la kawaida sana, lakini mwamini kutambua kwamba, ameitwa kuwa Mkristo Mkatoliki, ni jambo ambalo linapita ufahamu na matamanio yake ya kibinadamu.
Kuwa Mkatoliki wa kweli haimaanishi kufuata sheria na kanuni zinatolewa na Mama Kanisa, bali ni kutambua kwamba, Mwenyezi Mungu ameandaa njia makini inayopania kujenga na kuimarisha uhusiano na upendo wa dhati; kwa kujitoa bila ya kujibakiza.
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita anasema, uhusiano huu unajikita katika Fumbo la Msalaba, linaloonesha upendo wa Mungu kwa binadamu; upendo unaomkirimia mwanadamu utimilifu wa maisha yake na kumwokoa kutoka katika lindi la dhambi na mauti.
Askofu msaidìizi Leuzzi anayasema haya katika barua yake ya kichungaji kwa wanafunzi wa Vyuo Vikuu vilivyoko Roma. Anakumbusha kwamba, mwanadamu anaweza kuanza kumtafuta Mwenyezi Mungu kwa njia ya kazi ya uumbaji ambayo kimsingi inachapa ya Mungu mwenyewe; kwa kujiuliza maana ya maisha na Fumbo la Kifo.
Lakini ikumbukwe kwamba, kwa njia ya Yesu Kristo, Mwenyezi Mungu amejitaabisha kumtafuta mwanadamu katika mapito yake kabla ya mwanadamu mwenyewe kuanza kumtafuta Mwenyezi Mungu. Furaha ya kweli ni pale mwamini anapomtambua Kristo kuwa ni Bwana na Mwalimu, kama alivyofanya Mtakatifu Magdalena, alipokutana na Yesu Mfufuka!
Kuna ”vigogo” waliotema cheche na sera zilizokuwa zinapania kwa namna ya pekee kumpatia uhuru mwanadamu kutokana na vifungo vya kidini; kama ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia unavyotaka kuwasadikisha watu wa nyakati hizi, bila kusahau pia kwamba, hata elimu inaweza kumtumbukiza mwamini katika ombwe hili. Mwenyezi Mungu daima amemwacha mwanadamu katika uhuru wake na wala hakutaka kumfunga na sheria na utashi wa kumpenda na kujitoa kwake bila ya kujibakiza.
Mwenyezi Mungu amependa kumwonjesha mwanadamu upendo wake, kama sehemu ya mchakato unaopania kujenga na kuimarisha uhusiano wa dhati kati ya mwamini na Mwenyezi Mungu. Huu ndio uhuru unaoonesha katika kupenda na wala si kuwa mtumwa katika kupenda! Upendo wa Kristo unamwongoza mwamini katika uhuru kamili dhidi ya upendo ambao wakati mwingine ni kama ndoana; nipe nikupe!
Anampenda mwanadamu kutoka katika undani wake, ili kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano. Kristo anapenda kwa sababu anasukumwa na upendo unaomkirimia mwamini uhuru kamili, ili aweze kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya huduma kwa Mungu na jirani kama alivyofanya Mtakatifu Augustino, Askofu na Mwalimu wa Kanisa.
Waamini wanaanza hija ya ukombozi kwa kupakwa majivu na itakamilika katika Kesha la Pasaka, pale Mwenyezi Mungu atakapomshangaza mwanadamu kwa kumfufua Yesu kutoka katika wafu. Kila mtu anapaswa kutambua kwamba, ana thamani kubwa machoni pa Mungu, kwani ameumbwa kwa sura na mfano wake. Kila mtu yuko huru, kupenda na kuhudumia pamoja na kuwa mdau katika mapambano ya maisha yake kiroho na kimwili katika historia.
Wanafunzi wa vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu wanakumbushwa kuwa, katika hija ya maisha yao kuna Kiongozi na Mwalimu anayewaonesha dira na njia ya kupitia, changamoto kama ilivyokuwa kwa Mtakatifu Augustino, kusimama kidogo, kutafakari na kumpokea Kristo, bila shaka kila mmoja wao, atafurahia kuwa Mkristo Mkatoliki, si tu kwa maneno, bali kwa njia ya ushuhuda wa maisha yake!








All the contents on this site are copyrighted ©.