Serikali ya Brazil yamkaribisha Papa Francisko kushiriki Maadhimisho ya Siku ya Vijana
Duniani, 2013
Rais Dilma Rousseff wa Brazil ni kati ya viongozi wakuu wan chi waliohudhuria Ibada
ya Misa Takatifu, wakati Papa Francisiko alipokuwa anaanza utume wake kama Askofu
wa Jimbo la Roma hapa mjini Vatican hivi karibuni. Katika mazungumzo
ya faragha, Rais Rousseff alimwalika kwa mara nyingine tena Baba Mtakatifu Francisko
kutembelea Brazil wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa mwaka 2013 itakayofanyika
mjini Rio de Janeiro kuanzia tarehe 23 hadi tarehe 28 Julai 2013. Inakadiriwa
kwamba, zaidi ya Vijana million 4 kutoka sehemu mbali mbali za dunia watashiriki katika
tukio hili la Imani kati ya Vijana na Kanisa. Katika mkutano wa viongozi hawa wawili,
Baba Mtakatifu alimpatia zawadi Rais wa Brazil, Kitabu chenye mkusanyiko wa hati za
Mkutano mkuu wa Aparecida, kama matunda ya mkutano mkuu wa tano wa Shirikisho la Mabaraza
ya Maaskofu Katoliki Amerika ya Kusini na Caribbean uliofanyika mjini Aparecida, Brazil,
mwezi Mei 2007. Nakala ya Kitabu hiki alipewa pia alipewa Rais Cristina Fernàndes
de Kirchner wa Argentina. Itakumbukwa kwamba, Kardinali Jorge Mario Bergoglio alichangia
sana katika kukusanya maoni na hatimaye, kuchapisha kitabu hiki ambacho kwa sasa ni
rejea katika maisha na utume wa Kanisa. Itakumbukwa kwamba, Baba Mtakatifu mstaafu
Benedikto wa kumi na sita, alipofanya hija yake ya kwanza Amerika ya Kusini, alitumia
fursa hii pia kufungua mkutano wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Amerika
ya Kusini na Caribbean uliojikita zaidi katika changamoto za Uinjilishaji katika ulimwengu
mamboleo. Kitabu hiki kimesheheni tafakari za kichungaji zilizofanyiwa upembuzi yakinifu
katika maisha na utume wa Kanisa Amerika ya Kusini mintarafu hali ya Kijamii kwa sasa.
Baraza la Maaskofu Katoliki Brazil linasema Shirika la Habari za Kanisa Zenit
kwamba, linaendelea kushirikiana na Vatican katika kupanga ratiba rasmi la Maadhimisho
ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013. Kwa wakati muafaka, Baba Mtakatifu Francisko
atatoa ratiba ya hija yake ya kichungaji nchini Brazil kwa ajili ya Maadhimisho ya
Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013.