2013-03-26 11:07:01

Jumuiya ya Kimataifa inapaswa kushikamana ili kudhibiti biashara ya silaha kimataifa


Askofu mkuu Francis Chullikatt, Mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye Umoja wa Mataifa, akishiriki katika mkutano kuhusu mkataba wa biashara ya silaha kimataifa, anawaalika wajumbe kushirikiana kwa pamoja ili hatimaye, Jumuiya ya Kimataifa iweze kuandika ukurasa mpya wa historia kwa kupitisha mkataba huu. Lengo ni kujenga mazingira yatakayosaidia kudumisha amani na utulivu; mwanadamu akipewa kipaumbele cha kwanza.

Tangu awali, ujumbe wa Vatican kwenye mikutano kama hii, umekuwa ukikazia umuhimu wa Jumuiya ya Kimataifa kudhibiti biashara ya silaha kimataifa kupelekwa kwenye maeneo ambayo yana migogoro, kinzani na vita, kwani uwepo wa silaha hizi umekuwa ni chanzo kikubwa cha uvunjaji wa haki msingi za binadamu. Mafao ya kiuchumi yamekuwa yakipewa kipaumbele cha kwanza dhidi ya maisha ya binadamu na familia yake.

Ni wajibu kwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha kwamba, wanatekeleza kwa dhati makubaliano haya ya Umoja wa Mataifa katika udhibiti wa biashara ya silaha kimataifa. Badala ya kuwa na kikundi cha watu wachache wanaodhulumiwa, ujumbe wa Vatican unapenda kupanua wigo ili watu wengi zaidi waweze kufaidika na ulinzi unaobainishwa kwenye Mkataba huu.

Kundi hili linawagusa: wanawake na wanaume; watoto, wazee na walemavu; wakimbizi na watu wasiokuwa na makazi maalum; makabila na dini zenye waamini wachache. Wote hawa wanapaswa kulindwa dhidi ya biashara haramu ya silaha inayopelekea uvunjwaji wa haki msingi za binadamu na sheria. Mkutano wa Umoja wa Mataifa kuhusu silaha unatarajiwa kufungwa rasmi hapo tarehe 28 Machi 2013, huko New York, Marekani, kwenye Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa.







All the contents on this site are copyrighted ©.