Kardinali Pengo aadhimisha Ibada ya Jumapili ya Matawi Jimboni Zanzibar na kutoa salam
za Papa Francisko
Baba Mtakatifu Francisiko hivi karibuni, alikutana na kuzungumza na wawakilishi wa
dini na madhehebu kutoka sehemu mbali mbali za dunia, akikazia kwa namna ya pekee
majadiliano katika upendo na ukweli na kwamba, Kanisa Katoliki linapania kujenga na
kuimarisha majadiliano ya kidini na kiekumene na waamini wa dini na madhehebu mbali
mbali ya Kikristo. Kanisa linapenda kujielekeza pia katika majadiliano na wale wasiokuwa
na dini maalum, ambao daima wana kiu ya kutaka kumfahamu Mungu kutoka katika undani
wao.
Baba Mtakatifu Francisiko anakumbusha kwamba, Wakristo na Waislam wana
mwamini Mungu mmoja, aliye hai ambaye pia ni mwingi wa huruma na upendo; waamini wa
dini hizi wanamwendea wote kwa njia ya sala, changamoto ya kujenga na kudumisha ushirikiano
wa dhati baina ya Wakristo na Waislam kwa ajili ya mafao na ustawi wa binadamu wote.
Kuna haja ya kuendeleza urafiki na heshima kila mtu; daima wakisimama pamoja kulinda
na kutetea kazi ya uumbaji ambayo mwanadamu amedhaminishwa na Mwenyezi Mungu.
Wakristo
na Waislam anasema Baba Mtakatifu Francisko, wanaweza kujibidisha zaidi kwa ajili
ya kuwahudumia maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii; kwa kujikita katika
upatanisho na ujenzi wa amani ya kudumu; lakini jambo la msingi ni kushirikiana kwa
pamoja ili kuzima kiu ya uwepo wa Mungu inayooneshwa na watu kutoka sehemu mbali mbali
za dunia.
Hii ndiyo changamoto ambayo Kardinali Polycarp Pengo, Askofu mkuu
wa Jimbo kuu la Dar es Salaam aliyopeleka Jimboni Zanzibar, katika Maadhimisho ya
Jumapili ya Matawi, ambayo kwa mwaka huu, ilikuwa na nafasi ya pekee katika moyo wa
Baba Mtakatifu Francisko aliyemtuma Kardinali Pengo kumwasilishia salam na matashi
mema kwa Wakristo wa Zanzibar ambao wamepitia kipindi kigumu katika miaka ya hivi
karibuni.
Kardinali Pengo katika mahubiri yake, kwenye Kanisa Katoliki la Mtakatifu
Yosefu, Jimbo Katoliki la Zanzibar, amekazia kwa mara nyingine tena umoja, upendo
na mshikamano miongoni mwa wafuasi wa dini mbali mbali nchini Tanzania na kamwe tofauti
zao za kiimani zisiwe ni chanzo cha vurugu na chokochoko za kiimani. Hakuna mtu anayeweza
kuhalalisha mauaji ya binadamu mwingine kwa madai ya kwamba, anatetea imani kwa Mungu
aliye asili na uhai.
Kardinali Pengo ametumia fursa hii pia kuwataka Wazanzibar
kutunza mazingira kwa ajili ya mafao ya sasa na yale ya kizazi kijacho. Kuna wakati
Zanzibar ilikuwa inatoa maji safi ya kunywa, lakini sasa maji mengi ni ya chumvi.
Utunzaji wa mazingira ni jambo linalopaswa kupewa msukumo wa pekee na Jamii na wala
hawapaswi kulipuuzia.