2013-03-23 09:15:57

Juma Kuu: Kumbu kumbu ya Mateso, Kifo na Ufufuko wa Kristo


Kanisa linakianza kipindi cha Jumaa kuu, linalowapatia waamini fursa ya kuweza kutafakari kwa kina kuhusu mateso, kifo na ufufuko wa Kristo. Jumapili ya Matawi, Kanisa linakumbuka siku ile Yesu, Masiha alipoingia mjini Yerusalem akiwa amepanda Punda, alama ya unyenyekevu wa hali ya juu kabisa, huku watoto wa Wayahudi wakitandaza nguo zao njiani.
Ni Siku ya Vijana Kijimbo! Ni matumaini ya Kanisa kwamba, vijana kutoka katika Parokia mbali mbali pale inapowezekana, washerehekee siku hii wakiwa wamemzunguka Askofu wa Jimbo lao. Hata katika ngazi ya Kiparokia, vijana wanaweza kuiadhimisha Siku hii kwa kumzunguka Paroko wao! Kama mwaka huu hamkuweza kufaulu, basi jipangeni sawasawa hapo mwakani!
Waamini hata katika mapambazuko ya Millenia ya tatu, wanaendelea kuandamana huku wakimshangilia Kristo Mfalme wa amani, huku wakiwa wamebeba matawi ya mitende mikononi mwao; matawi yanayohifadhiwa kwa heshima, kama kumbu kumbu ya kuonesha uaminifu wao kwa Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu!
Hiki ni kipindi cha tafakari ya kina, hasa wakati huu Mama Kanisa anapoendelea kuadhimisha Mwaka wa Imani, changamoto kwa kila mwamini kuhakikisha kwamba, anaifahamu imani yake, ili aweze kuikiri, kuiadhimisha, kuimwilisha katika matendo adili na hatimaye, kuisali, kama sehemu ya mchakato wa imani tendaji.
Mara mbili kwa mwaka, Mama Kanisa anawapatia Watoto wake fursa ya kuweza kusikiliza Mateso ya Bwana Wetu Yesu Kristo yakisomwa kwa Ibada kubwa: Ijumaa kuu na Jumapili ya Matawi. Liturujia ya Jumapili ya Matawi, inaanza kwa kumshangilia Kristo, Hosana Mwana wa Daudi na baadaye, tunahitimisha kwa kusema, mwondoe, mwondoe, Msulubishe!
Hapa Yesu anatualika kushiriki katika ile Saa yake ya mateso, ambayo kwa hiyari yake mwenyewe, anaamua kujitosa kimasomaso kuteswa na kufa Msalabani na hatimaye, kufufuka siku ya tatu, kwa ajili ya ukombozi wa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti.
Huu ndio mwanzo wa Injili unaojikita katika mateso, kifo na ufufuko wa Yesu. Wasifu wa watu maarufu katika ulimwengu wetu unaanza kwa siku yake ya kuzaliwa hadi pale anapoitupa mkono dunia! Lakini, kwa Yesu, wasifu wake unaanza katika mateso, kifo na ufufuko wake. Hii ndiyo hazina ya Imani ambayo vijana wanapaswa kurithishwa, kama anavyokazia Baba Mtakatifu Francisko kwa Kanisa. Kifo cha Yesu kimetokana na dhambi za binadamu, ni wakati wa kukinywea kile Kikombe cha mateso.
Mateso ya Yesu yanawahusisha watu wengi: Yuda Iskarioti aliyemsaliti kwa busu! Mtakatifu Petro aliyemkana mara tatu, Mitume waliotimua mbio walipoona amekamatwa na kukokotwa kuelekea hukumuni, Pilato aliyenawa mikono akisema hausiki kabisaaa na kifo cha Yesu, hata kama hakumkuta na hatia, lakini amestahili kufa! Huu ndio mwelekeo wa wale wanaopindisha sheria kwa ajili ya mafao yao binafsi! Baraba anayeponea chupu chupu kutoka katika tundu la sindano! Wevi wawili waliokuwa wametundikwa Msalabani.
Katika Njia ya Msalaba kuelekea Mlimani Kalvari, nje ya Mji, kulikuwepo na wanawake wa Yerusalemu waliokuwa wanamlilia Yesu na pale chini ya Msalaba alikuwepo Bikira Maria amesimama kwa ukimya. Kuna wengine waliokuwa mbali wanachungulia kuona kama Yesu atawafanyia Suprise! Lakini, maskini, wakati huu, Yesu akaamua kubaki Msalabani, ili kuchukua dhambi za binadamu.
Kati ya wahusika mbali mbali tuliowasikia katika Simulizi la Mateso ya Yesu, jiulize wewe uko sehemu gani? Tunaweza kufunga Injili ya Mateso ya Yes una kurudi nyumbani kama walivyofanya wale watesaji na mashahidi waliokwisha fariki dunia kitambo kirefu kilichopita. Pilato amekwisha ondoka mahakamani pamoja na wazee wa Baraza.
Lakini, mchakato wa hukumu ya Yesu bado unaendelea miongoni mwa Wakristo wanaokumbana na madhulumu kutokana na imani yao kwa Kristo na Kanisa lake; unaendelea kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii; hukumu hii inaendelea kwa wote wanaokumbatia utamaduni wa kifo na uharibifu wa mazingira. Hukumu inaendelea kwa wote tunao endelea kutenda dhambi.
Simulizi la Mateso ya Yesu Kristo litukumbushe mambo makuu matatu: Mateso, Kifo na Ufufuko wa Kristo; changamoto ya kuifahamu Kanuni ya Imani, ili tuweze kuiadhimisha kwa ushiriki mkamilifu, hali tukijitahidi kuimwilisha katika matendo adili kwa kutambua kwamba, hii ni imani ambayo tunaisali kama kielelezo cha ile imani tendaji ambayo ni dira na mwongozo wa maisha yetu.
Ninakualika kuchukua Msalaba wako kila siku ya maisha yako na kuanza kumfuasa Yesu Kristo, changamoto ya kupyaisha imani yetu katika hija ya maisha yetu! Jamani, kesheni pamoja na Kristo anapoanza Njia ya Msalaba!
Na Padre Richard Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.