2013-03-23 09:49:42

Askofu Mkude: Waamini shindeni Ubaya kwa njia ya kutenda wema, mkionesha imani thabiti kwa Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka!


Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, iwe ni fursa makini kwa waamini kuifahamu, kuikumbatia, kuishuhudia na kuwashirikisha wengine, ili waweze kumfahamu, kumpenda na kumtumikia Kristo katika hija ya maisha yao ya kila siku. RealAudioMP3

Ni changamoto ya kukuza na kuendeleza zile ahadi za ubatizo ambazo waamini wanaapa wao wenyewe au kwa niaba yao! Vinginevyo, imani kwa Kristo na Kanisa lake, inaweza kuzimika kama kibatari na watu kuanza kuogelea katika giza la mauti na kifo!

Ni changamoto iliyotolewa na Askofu Telesphor Mkude wa Jimbo Katoliki Morogoro, wakati wa Ibada ya Kubariki Krisima ya Wokovu, iliyofanyika kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Patris, Jimboni Morogoro. Kimapokeo Ibada hii hufanyika Siku ya Alhamisi Asubuhi, Mapadre pamoja na Waamini hushiriki katika Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kubariki mafuta matakatifu yaani "Krisma ya Wokovu" yatakayotumika kwa ajili ya Sakramenti ya Ubatizo, Kipaimara, Daraja Takatifu na Mpako wa Wagonjwa.

Lakini kutokana na changamoto za kichungaji, Majimbo mengi huiadhimisha Siku hii kabla, ili kutoa nafasi kwa Mapadre kuadhimisha Alhamisi kuu kwa utulivu, wakikumbuka Siku ile Yesu alipoweka Sakramenti ya Ekaristi Takatifu na Upadre, akawataka wazimwilishe Sakramenti hizi kwa njia ya huduma kwa ndugu zao katika Kristo, lakini zaidi kwa wanyonge na wale wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Katika mahubiri yake kwa mujibu wa Radio Ukweli ya Jimbo Katoliki Morogoro, Askofu Mkude amesema kwamba, watu wengi wanamezwa na malimwengu, kiasi cha kukumbatia na kutoa kipaumbele cha pekee katika mali na madaraka, kiasi cha kufisha maagano yao na Mwenyezi Mungu. Watu wa namna hii ni sawa na taa iliyozimika.

Kipindi cha Kwaresima iwe ni fursa ya kutubu na kumwongokea Mwenyezi Mungu; watu watumie nafasi zinazotolewa na Mama Kanisa ili kujipatanisha na Mungu pamoja na jirani zao, ili dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi. Katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani uliotangazwa na kuzinduliwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, waamini wajitahidi kutolea ushuhuda imani yao kwa njia ya matendo ya huruma hasa zaidi kwa maskini wa kiroho na kimwili na wote wanaohitaji kuonjeshwa huruma na upendo wa Mungu. Kwa njia hii, waamini watakuwa wanajiwekea hazina mbinguni.

Kuhusu vurugu za kidini nchini Tanzania, Askofu Mkude anawaalika waamini kushinda ubaya kwa wema. Kwa njia hii waamini na watu wote wenye mapenzi mema wanaweza kudumisha na kuimarisha amani nchini Tanzania; amani ambayo kwa miaka ya hivi karibuni imeanza kumeguka vipande vipande kutoka na chokochoko za kidini.







All the contents on this site are copyrighted ©.