2013-03-22 10:32:06

Upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama ni matokeo ya ushirikiano wa kimataifa


Jumuiya ya Kimataifa tarehe 22 Machi 2013 inaadhimisha Siku ya Maji Kimataifa. Wataalam wa masuala ya maji na afya, chakula na lishe; umaskini na mazingira; ubaguzi na nyanyaso dhidi ya wanawake; mwendelezo wa usawa na demokrasia ya kweli; kwa pamoja wanapenda kuunganisha sauti zao kwa kusema maji ni uhai na mhimili mkuu katika medani mbali mbali za maendeleo na maisha ya mwanadamu.

Kwa bahati mbaya maji sasa inaonekana kuwa ni bidhaa adimu inayotafutwa kwa udi na uvumba katika soko la kitaifa na kimataifa, lakini kwa bahati mbaya, kuna mamillioni ya watu ambao bado hayana uhakika wa maji safi na salama. Jopo la watetezi wa haki msingi za binadamu linasema, kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kutenga rasilimali itakayosaidia watu kutoka katika nchi zinazoendelea duniani kuwa na uhakika wa maji safi na salama, kwa ajili ya maboresho ya huduma ya afya; upatikanaji wa chakula pamoja na mapambano dhidi ya umaskini wa kipato na hali.

Kuna haja pia ya Jumuiya ya Kimataifa kuibua na kutekeleza mikakati ya utunzaji bora wa mazingira kwa ajili ya kizazi cha sasa na kile kijacho, ili kuendelea pia kuwa na uhakika wa upatikanaji wa maji kwa ajili ya maboresho ya afya; jambo linalohitaji ushirikiano wa dhati, sanjari na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Serikali hazina budi kutoa msukumo wa pekee kwa upatikanaji wa maji kutokana na ukweli kwamba, waathirika wakuu wa ukosefu wa maji au umbali wa upatikanaji wa maji ni wanawake. Maji ni sehemu ya haki msingi za binadamu na wala si tu bidhaa au huduma!

Wataalam wa haki msingi za binadamu wanaialika Jumuiya ya Kimataifa kuadhimisha Siku ya Maji Kimataifa, kwa kuweka mikakati ya matumizi bora ya maji yaliyopo pamoja na kubainisha mbinu zitakazotumiwa ili watu wengi zaidi waweze kupata maji safi na salama kwa ajili ya ustawi na maendeleo yao







All the contents on this site are copyrighted ©.