Papa akutana na kuzungumza na Waziri Mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda mjini Vatican
Waziri mkuu Mizengo Pinda wa Tanzania amekutana na Papa Francisko na kufanya naye
mazungumzo ya faragha ikiwa ni pamoja na kuwasilisha salamu za pongezi kutoka kwa
Rais Jakaya Kikwete.
Waziri Mkuu alipata fursa hiyo Alhamisi, Machi 21, 2013
alipofika kwenye makazi ya muda ya Papa Francisko yaliyoko Domus Sanctae Marthae mara
baada ya kumaliza vikao na wawakilishi kadhaa wa mashirika ya kimataifa walioko mjini
Roma, Italia.
Katika mazungumzo yao, Waziri Mkuu alimweleza Papa Francis kwamba
amefika kuwasilisha salamu za pongezi kutoka kwa Rais Kikwete. Katika salamu hizo,
Waziri Mkuu Pinda alisema: “Rais wa Tanzania, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete anakutakia
heri katika jukumu hili jipya ulilopewa na Mwenyezi Mungu. Tunamshukuru Mungu kwa
kukupa jukumu la kulea Kondoo wa Kristo, nasi tutaendelea kukuombea katika utume huu
mkubwa ulionao.”
Waziri Mkuu alimweleza Papa Francisko kwamba, Rais Kikwete
alitamani kuwepo kwenye ibada yake ya kusimikwa rasmi lakini kutokana na majukumu
mengine ya kitaifa aliyokuwa nayo, hakuweza kufika na badala yake amemuomba Waziri
Mkuu amuwakilishe.
Akipokea salamu hizo, Papa Francisko alisema anatambua fika
jinsi Tanzania inavyojitahidi kuendeleza amani chini ya uongozi wa Rais Jakaya Kikwete.
“Tutaendeleza ushirikiano wa karibu uliokuwepo baina ya nchi zetu,” alimalizia Papa
Francisko.
Waziri Mkuu Pinda na ujumbe wake, walipata pia nafasi ya kuonana
na Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican.
Wakati huo huo,
Waziri mkuu Pinda wakati wa ziara yake mjini Roma alipata nafasi ya kukutana na kuzungumza
pia na Mkurugenzi mkuu wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa, FAO, Bwana
Josè Graziano da Silva, kwenye Makao Mkuu ya FAO, hapa mjini Roma. Alitembelea pia
Ofisi za Shirika la Mpango wa Chakula Duniani, WFP siku ya Jumatano, tarehe 20 Machi
2013.