2013-03-21 09:04:32

Wananchi wa Zimbabwe wanaunga mkono Katiba Mpya kwa 95%


Asilimia 95% ya wananchi wa Zimbabwe wanaunga mkono muswada wa Katiba Mpya ya Zimbabwe. Haya ni matokeo ya kura ya maoni iliyopigwa nchini Zimbabwe mwishoni mwa juma. Lengo ni kupunguza madaraka makubwa ya Rais, ambaye ataweza kuwaongoza wananchi wa Zimbabwe kwa vipindi viwili tu!

Kwa upande wake, Rais Robert Mugabe, mwenye umri wa miaka 89 bado anaruhusiwa kikatiba kuwaongoza wananchi wa Zimbabwe, kwani sheria hairudi nyuma, ingawa Rais Mugabe amekuwepo madarakani tangu mwaka 1980, Zimbabwe ilipojinyakulia uhuru wake kutoka kwa Waingereza.

Upatikanaji wa katiba mpya ni hatua kubwa ya maendeleo ya kidemokrasia na utawala bora ambao umewagharimu sana wananchi wa Zimbabwe katika kipindi cha miaka michache iliyopita! Zimbabwe iliyokuwa inajivunia maendeleo na ustawi wa wananchi wake, ikajikuta inachechemea katika kinzani na misigano ya kisiasa na kijamii; matukio yaliyokwamisha mchakato wa maendeleo endelevu nchini Zimbabwe.

Katiba Mpya ya Zimbabwe inatoa madaraka makubwa kwa Bunge la Zimbabwe ambalo kwa sasa lina idadi kubwa ya Wabunge kutoka katika Chama cha Upinzani. Kimsingi, Katiba inatoa kipaumbele cha kwanza kwa heshima na utu wa binadamu, haki msingi, uhuru wa mtu, dhamiri pamoja na uhuru wa mtu kujieleza. Hadi kufikia hatua hii, wananchi wa Zimbabwe wametoka jasho kweli kweli!







All the contents on this site are copyrighted ©.