2013-03-19 10:59:44

Papa Francisko ni nyota ya matumaini kwa wakimbizi na wahamiaji, wenye kiu na njaa ya haki, amani, msamaha na upatanisho!


Mheshimiwa Padre Peter Balleis, Mkurugenzi mkuu wa Shirika la Wayesuit kwa ajili ya kuwahumia wakimbizi anasema, wamepokea kwa mikono miwili habari za kuchaguliwa kwa Baba Mtakatifu Francisko kuwa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Ni kiongozi ambaye ameonja hadha ya kuishi uhamishoni, kumbe atakuwa ni kielelezo cha matumaini kwa wakimbizi na watu wasiokuwa na makazi maalum wanaonesha kiu na njaa ya haki, amani, upendo na mshikamano wa dhati.

Hili ni kundi kubwa la watu wanaotaka kuonja upendo na msamaha wa kweli, mambo ambayo Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kuyakazia katika maisha na utume wake. Anatoa mwaliko kwa Kanisa kuhakikisha kwamba, linawashirikisha wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, ili waweze kuona huruma na upendo wa Mungu katika maisha yao.

Hawa ni wale ambao Shirika la Wayesuit kwa ajili ya kuhudumia wakimbizi limekuwa likitenda kama sehemu ya utume wake. Ikumbukwe kwamba, waathirika wakubwa ni wanawake na watoto, wanaopaswa kweli kupewa kipaumbele cha kwanza; kwa kuheshimu na kuthamini utu wao kama binadamu walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuanza safari ya udugu na upendo miongoni mwa Jumuiya ya Kimataifa. Hii ndiyo changamoto ambayo Baba Mtakatifu Francisko anapenda pia kuwashirikisha waamini wote kama njia ya kukuza na kuimarisha haki inayojionesha katika imani tendaji.

Unyenyekevu, upole na umakini kwa wote wanaoteseka ni kati ya fadhila ambazo Mwenyezi Mungu amemkirimia Papa Francisko, ambaye ameguswa na mateso na mahangaiko ya wananchi wa Argentina.

Wayesuit wanasema, kuna watu wengi wenye kiu na njaa ya haki, njaa ya ulinzi na usalama, wanaohitaji kuonja upendo na msamaha wa kweli, ili kwa pamoja waweze kusimama kidete kulinda na kutetea: mafao ya wengi, utu na heshima ya binadamu. Ni matumaini ya wengi kwamba, Baba Mtakatifu Francisko atasaidia kuwaonjesha watu waliokata tamaa katika maisha, matumaini na upendo unaobubujika kutoka kwa Kristo, mchungaji mkuu.







All the contents on this site are copyrighted ©.