2013-03-19 08:58:30

Papa Francisko anawachangamotisha waamini Kuinjilisha kwa njia ya matendo!


Kardinali Fernando Filoni, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa Watu anasema kwamba, changamoto kubwa inayotolewa na Baba Mtakatifu Francisco wakati huu anapouanza rasmi utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro ni kujitosa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Uinjilishaji Mpya, kwa njia ya ushuhuda wa imani tendaji.

Ni mwaliko wa kuwaendea watu mahali walipo, ili waweze kuonja kwa mara nyingine tena ile furaha ya Habari Njema ya Wokovu inayopata chimbuko lake kwa Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu.

Kardinali Filoni anasema, kwa sasa Mama Kanisa anawachangamotisha waamini kujitosa kwa ari na bidii zaidi kumtangaza Kristo, hasa kwa njia ya huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii; hawa wanapaswa kuonjeshwa huruma na upendo wa Kristo.

Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kuwahimiza Makleri na Familia ya Mungu kwa ujumla, kujiondoa kutoka katika ubinafsi, raha na starehe na kuanza hija ya kuwatangazia watu upendo, furaha na matumaini, kwa wote wale wanaoogelea katika dimbwi la umaskini wa kipato na maisha ya kiroho!

Kardinali Filoni anawaalika waamini kuonesha mshikamano na upendo wa pekee kwa Baba Mtakatifu Francisko kwa njia ya huduma kwa maskini. Baba Mtakatifu Francisco amekuja kwa wakati wake, Mama Kanisa anapoendelea na hija ya kutangaza Injili ya Kristo hadi miisho ya dunia. Haya ni matunda ya sala na kazi ya Roho Mtakatifu, iliyowawezesha Makardinali katika mkutano wa uchaguzi.

Huu ndio ushuhuda uliotolewa na Mama Theresa wa Calcutta enzi ya uhai wake, ushuhuda wa Injili unaotekelezwa na waamini sehemu mbali mbali za dunia. Jina la Mtakatifu Francisko wa Assisi linaonesha fadhila ya unyenyekevu, ari na moyo wa Uinjilishaji.







All the contents on this site are copyrighted ©.