2013-03-18 07:43:17

Kwaresima ni kipindi cha Mshikamano wa upendo


Patriaki Bartolomeo wa kwanza wa Kanisa la Kiorthodox katika maadhimisho ya Kipindi cha Kwaresima kwa Kanisa la Kiorthodox anawaalika waamini kuonesha upendo na mshikamano na maskini pamoja na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kutokana na hali yao ya maisha. Mshikamano huu ni muhimu sana kwa mwaka huu wa 2013, ambao kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa, umetangazwa kuwa ni Mwaka wa Mshikamano wa Kimataifa. Ni mwaliko wa kushirikishana na kugawana kile kidogo ambacho Mwenyezi Mungu amewakarimia waja wake.

Katika ujumbe wake kwa Jumapili ya Msamaha, ambayo imeadhimishwa na Kanisa la Kiorthodox, Jumapili, tarehe 17 Machi 2013, anawaalika waamini kwa namna ya pekee kuonesha upendo kwa jirani zao, ili kujitajirisha katika maisha ya kiroho. Ni mwaliko na changamoto ya kutosheka na kipato chao, waaminifu na waadilifu wa mali ya umma. Kwa maneno machache anasema Patriaki Bartolomeo wa kwanza, waamini wanapaswa kutolea ushuhuda wa maisha adili.

Lakini kwa bahati mbaya, ulimwengu mamboleo unaonesha sura tofauti kabisa kwa watu kupenda mno mali, utukufu na madaraka. Katika mahubiri yake, Mtakatifu Yohane Chrisostom anasema, hakuna jambo baya kuliko yote ikiwa kwa mtu kutojua kupenda. Kwa mwelekeo huu wa maisha, hakuna mtu anayeweza kuguswa na shida pamoja na mahangaiko ya jirani zake. Waamini wajifunze kutekeleza matendo ya huruma katika maisha yao, kwa kuwaonesha jirani zao upendo, huruma na faraja.

Patriaki Bartolomeo wa kwanza katika mahubiri yake anabainisha kwamba, hakuna furaha kubwa kama ile ya mtu kumwonjesha upendo jirani yake. Kwa bahati mbaya, mwalimu dunia anapenda kuwafundisha vijana kupenda raha na anasa hata kupita kiasi, hali ambayo inapelekea kinzani na migawanyiko katika Jamii. Jamii ijifunze kuonesha moyo wa upendo na mshikamano wa kweli, kwa kusaidiana kwa hali na mali.

Kwaresima kiwe ni kipindi cha kusafisha roho na mwili kwa kujikita zaidi katika upendo kwa Mungu na jirani; upendo ambao Yesu mwenyewe amewaonesha wafuasi wake. Upendo huu hauna budi kuwa ni sehemu ya sadaka na majitoleo ya waamini na watu wote wenye mapenzi mema. Upendo ujioneshe katika matendo, hasa kwa wakati huu, watu wengi wanapoendelea kuonja athari za mtikisiko wa uchumi kimataifa.








All the contents on this site are copyrighted ©.