Harambee kuchangia ukarabati wa Parokia ya Magomeni, Jimbo kuu la Dar es Salaam
Waziri mkuu Mizengo Pinda wa Tanzania, ameongoza harambee ya papo kwa papo na kufanikiwa
kukusanya sh. milioni 31.5 zikiwa ni ahadi na fedha taslimu kwa ajili ya ukarabati
wa Kanisa la Parokia ya Mashahidi wa Uganda, Jimbo kuu la Dar es Salaam.
Akizungumza
na waamini wa Parokia ya Magomeni, Jumapili, Machi 17, 2013, kabla ya kuendesha harambee
hiyo, Waziri Mkuu aliusifu uongozi wa Parokia ya Magomeni kwa kuamua kufanya upanuzi
wa Kanisa hilo ili liweze kuhudumia waamini wengi zaidi.
“Nia yao ni nzuri
sana na wameona mbali mapema. Magomeni hii ya leo si ya wakati ule, na wala haitakuwa
hivi katika miaka mingine 50 ijayo. Zamani usingeweza kuona hata ghorofa moja hapa
Magomeni lakini sasa hivi maghorofa hayahesabiki,” alisema.
Aliwasisitiza waamini
hao kujitoa kwa ajili ya kazi ya Kristo kwa sababu hakuna sadaka ambayo ni ndogo.
“Hakuna sadaka iliyo ndogo mbele ya Mungu, kikubwa ni dhamira tu. Kanisa ni letu na
litajengwa na sisi waamini ili mradi kila mmoja wetu aseme Kanisa hili nitalijenga,”
alisisitiza.
Mapema akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na waamini hao, Baba
Paroko wa Kanisa hilo, Padri Sixfrious Rwechungura alisema wameanza kazi ya ukarabati
tangu Agosti 15, 2011 na kwamba hadi sasa wamekwishakusanya sh. milioni 350 iliyotokana
na nguvu za waamini wenyewe bila msaada wa kutoka nje.
Alisema wanahitaji kiasi
cha sh. milioni 300 ili kukamilisha kazi hiyo ambayo inapaswa kukamilika katika miaka
miwili ijayo ili iendane na maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 ya Parokia ya Magomeni.
Katika
harambee hiyo, Waziri Mkuu na mkewe Mama Tunu Pinda waliahidi kuchangia sh. Milioni
10 na kutoa sh. Milioni mbili za kianzio. Pia aliendesha mnada wa mbuzi aliyenunuliwa
kwa sh. 600,000/- na mkoba ulionunuliwa kwa sh. 150,000/-.