2013-03-16 09:03:38

Shutuma dhidi ya Kardinali Bergoglio hazina msingi wowote!


Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, kampeni za kutaka kumchafua Kardinali Jorge Mario Bergoglio, ambaye kwa sasa ni Baba Mtakatifu Francis, zimechapishwa na gazeti moja ambalo linajipambanua kwa kampeni chafu za kutaka kuwapaka watu matope. Ni gazeti ambalo limekuwa likiendesha kampeni dhidi ya Makleri, kiasi kwamba, si jambo la kushangaza kusikia gazeti hili limeibuka kwa mara nyingine tena kutaka kumchafua Kardinali Bergoglio.

Shutuma zinazotolewa na gazeti hili zinapata chimbuko lake, wakati Bergoglio alipokuwa nchini Argentina kama Mkuu wa Shirika la Wayesuit, pale ambapo Mapadre wawili walipotekwa nyara na kwamba, hakuweza kutoa kinga dhidi ya Mapadre hao wasitekwe nyara.

Padre Lombardi anafafanua kwamba, shutuma hizi hazina msingi wowote. Vyombo vya sheria nchini Argentina wakati fulani vilimhoji kuhusu shutuma hizi, lakini hakuna hata siku moja vilipomkuta na hatia wala shitaka la kujibu. Mhusika mwenyewe alikana shutuma hizi na kuhifadhiwa.

Padre Lombardi anabainisha kwamba, kuna vielelezo na ushahidi mkubwa kutoka kwa watu mbali mbali wanaonesha kwamba, Bergoglio aliwalinda na kuwapatia hifadhi wakati wa madhulumu nchini Argentina, pale nchi ilipokuwa inatawaliwa kwa mtutu wa bunduki.

Mchango wa Bergoglio unafahamika sana, pale alipoteuliwa kuwa Askofu, alipoanzisha mchakato wa kuomba msamaha kwa ajili ya Kanisa la Argentina kwamba, wakati wa madhulumu, Kanisa Katoliki halikujishughulisha sana kuwalinda na kuwatetea wanyonge na wote waliokuwa wanadhulumiwa na utawala wa Kidikteta.

Shutuma hizi zinafumbatwa katika upembuzi yakinifu wa masuala ya kihistoria na kijamii wakati wa utawala wa kidikteta, zilizofanywa na makundi dhidi ya Makleri, kama njia ya kulishambulia Kanisa. Shutuma zote hizi hazina msingi na lazima zipingwe kwa kauli moja. Ndivyo Padre Federico Lombardi, Msemaji mkuu wa Vatican anavyohitimisha maneno yake dhidi ya shutuma zinazolenga kumpaka matope Kardinali Bergoglio.








All the contents on this site are copyrighted ©.