2013-03-16 08:42:53

Papa amtembelea Kardinali Jorge Mejia Hospitalini; wengi wapigwa na butwaa!


Baba Mtakatifu Francis, Ijumaa jioni, tarehe 15 Machi 2013 amemtembelea Kardinali Jorge Mejia, mwenye umri wa miaka 90, aliyepatwa ugonjwa wa moyo siku ya Jumatano tarehe 13 Machi 2013 na kulazimika kulazwa kwenye Hospitali ya Pius XI, iliyoko mjini Roma. Katika hotuba yake kwa Makardinali siku ya Alhamis, aligusia hali ya Kardinali Mejia na kusema kwamba, inaendelea vyema na alikuwa anawatakia matashi mema katika maisha na utume wao.

Kardinali Mejia alizaliwa Jimbo kuu la Buenos Aires na kwa miaka kadhaa alifanya utume wake mjini Vatican kama Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Maaskofu. Alikuwa Mkutubi mkuu wa Maktaba ya Kanisa Katoliki yenye utajiri mkubwa na nyaraka mbali mbali za Kanisa.

Baba Mtakatifu Francis ameifanya ziara hii inayokwenda sanjari na changamoto alizowapatia Makardinali katika mahubiri yake ya kwanza kama Khalifa wa Mtakatifu Petro kwa kusema kwamba, hawana budi kutembea, kujenga na kumshuhudia Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Wakati wa ziara yake binafsi Hospitalini hapo, Baba Mtakatifu Francis aliwaomba wafanyakazi wa Hospitali kusali kwa ajili yake.

Amewashukuru kwa kazi kubwa wanayoifanya kwa ajili ya kuwahudumia wagonjwa na wote wanaoteseka. Alipata nafasi ya kusali pamoja na baadhi ya watawa wanaohudumia Hospitalini hapo. Baadhi ya wafanyakazi waliposikia kwamba, Baba Mtakatifu Francis alikuwa Hospitalini hapo, walijitokeza kumlaki, kumsalimia na hatimaye, akawapatia baraka zake za kitume.







All the contents on this site are copyrighted ©.