2013-03-16 12:02:26

Kuweni macho na ahadi za kazi Ulaya


Katika makala haya yanayounga mkono kampeini kali dhidi ya utumwa mambo leo, na tuzamishe fikira zetu, katika kukitafakai kipindi cha tangu mapambazuko ya Uhuru kwa mataifa ya Afrika hadi leo hii ambamo mengi ymeadhimisha miaka hamsini ya kuutokomeza ukoloni. Tukiainisha pia na utekelezaji wa maazimio ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican (Vatican II) ambao mwaka huu pia tuna sherehekea kutimiza miaka 50 ya uwepo wake, na katika muono wa Azimio la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa.

Kama ilivyoelezwa katika dibaji ya hati za Mtaguso Mkuu wa pili wa Vatican, historia ya binadamu, daima husonga mbele na matukio ya utendaji wake wa kila siku , hadi hatima ya maisha ya mtu. Ni upigaji wa hatua katika mwendo wa maisha ambamo kwa wafuasi wa Kanisa, humulikiwa na mwanga mkuu wa Kristu “ binadamu mpya “ mwenye uwezo wa kuwaunganisha watu wa mataifa yote kuwa familia moja ya Mungu, katika hija hii ya maisha duniani. .

Baba Mtakatifu Yohane XX111, alipotangaza rasmi Mtaguso huu wa Vatican II, alisisitiza ulazima wa marekebisho mapya, si kurekebisha kanuni za imani zinazo dumu milele , ambazo ni mpya kila wakati, ila kutafakari upya upendo uliofumbatwa katika kweli za imani, uongofu, toba, unyenyekevu na kutangaza kwa nguvu habari njema ya kukombolewa na upendo wa Injili.

Historia ya Kanisa inatufundisha juu ya ukuu wa vipaji vya Mungu mwenyewe, ambavyo hufanya kazi ndani ya kanisa, katika kukabiliana na changamoto na matatizo mengi na ya aina mbalimbali katika harakati za kutekeleza maazimio yanayotajwa katika hati ya Vatican 11, mojawapo ikiwa azimio juu ya utume wa walei, katika mazingira ya kijamii.

Mtaguso II unasema, Utume wa walei katika mazingira ya Kijamii , unadai juhudi za kuipenyeza roho ya Kikristu ndani ya fikra na desturi , sheria na miundo ya jumuiya wanaoishi kama jukumu na faradhi ya walei. Katika uwanja huu, walei wanaweza kutimiza utume wa mtu kwa mwenzake aliye sawa na yeye. Na hivyo wanatimiza ushuhuda wa maisha, si kwa maneno tu lakini kimatendo katika mazingira ya kazi zao au amali au masomoni au maeneo ya starehe na viburudisho, na katika mifumo mingine ya maisha.( tz.962).

Walei wanatimiza utume huu wa Kanisa katika ulimwengu, kwanza kabisa kwa kuambatana na mwenendo wa imani , ambao kwa njia yake wanakuwa mwanga wa ulimwengu katika kushughulikia yote kwa moyo mnyoofu, na hivyo wanawavuta wengine kupenda ukweli na wema na hatimaye kulipenda kanisa na Kristu , kwa mapendo ya kidugu ambayo yanawawezesha kushiriki katika hali za maisha yote ya kazi, mateso na matumaini ya ndugu zao. Na hivyo inakuwa ni kuiandaa mioyo ya watu wote polepole, katika utayari wa kutendewa kwa neema inayoweza kuokoa(tz. 963).

Na hivyo nafasi ya utume wa walei kijamii, inapanuka na kuingia kwenye mipango ya kitaifa na kimataifa , walei kama wahudumu wa hekima za Kristu, katika kupenda asili ya uadilifu , uaminifu na wajibu wa raia mwema kulingana na haki na sheria na masharti yote ya Kimaadili na wema wote.


Kwa kukiri heshima ya asili na haki sawa isiyoweza kuondolewa kwa watu wote wa familia ya binadamu, inakuwa ni msingi wa uhuru, haki na amani duniani.


Katika misingi hiyo, turejeshwa katika mada: mapambano dhidi ya utumwa mambo leo ,ambao ni utendaji mbovu tunaoishi nao, pengine bila kujua lakini upo na ndivyo ilivyo. Kila siku watu wanachukuliwa na kupelekwa sehemu wasizo zijua kwa ahadi za uongo za kwenda kupata kazi au kuboresha masilahi yao na kumbe sivyo.

Na inafahamika wazi kwamba, kupuuza na kudharau haki za binadamu husababisha vitendo vya kishenzi ambavyo huzua vilio na ugandamizaji dhamiri ya mwanadamu, na matazamio yake ya kuifurahia dunia, kama mtu huru katika kujieleza na kuikiri imani yake, mtu aliye uhuru dhidi ya hofu na mashaka ya kugandamizwa na mwingine.

Watu wema, wanajali madhulumu hayo na kuona kwamba, ni wajibu kutetea na kulinda kisheria upinzani wote dhidi ya dhuluma na uonevu ulio kinyume na haki za binadamu. Na kuna ulazima wa kukuza hali zote za kujenga urafiki na maridhiano kati ya watu na mataifa, kama ilivyo tajwa katika hati ya Azimio la Umoja wa Mataifa. Nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa wameridhia imani hii katika haki za asili, heshima na thamani ya binadamu na katika usawa wa haki kwa wanaume na wanawake na kuwa na nia ya kukuza maendeleo ya kijamii yanayo pania kufanikisha hali bora za maisha kwa kila binadamu.

Linakuwa ni jambo la lazima, kwa kila mmoja kuwa msharika wa Umoja wa Mataifa, katika kukuza heshima , haki za binadamu na uhuru wa kimsingi. Uelewe huu wa pamoja wa haki na uhuru, una umuhimu mkubwa kwa ajili ya utambuzi kamili kwa ahadi hiyo ya Umoja wa Mataifa.

Hivi karibuni , Askofu Mkuu Giovanni Martinelli, Mtawala wa Kitume wa Jimbo la Tripoli Libya , akirejea wimbi la ghasia za wababe wa Kiislamu kushambulia wengine alisema, "katika ukweli wake, ubabe huo, ni matokeo ya kutojua maana ya uhuru wa mtu. Wengi wao wanadhani mtu kuwa, uhuru ,ni utendaji wa kiholela usiokuwa na sheria".Hilo pia , matokeo ya kukosa uzoefu wa kuishi katika hali za uhuru kamili kwamba uhuru daima huandamana na mipaka na kuheshimu wengine.

Ibara ya 1, katika makubaliano ya Umoja wa Mataifa inasema, watu wote wamezaliwa huru na sawa katika heshima na haki msingi zote za binadamu, na hivyo wanapaswa kutenda kwa mwelekeo wa roho ya udugu wa mmoja kwa mwingine.

Na Ibara 2 inasema, kila mmoja ana haki ya kuwa na haki zote na uhuru wote, bila ya ubaguzi wa aina yoyote, iwe rangi, jinsia, lugha, dini, maoni ya kisiasa au nyingine ya asili ya taifa au ya kijamii, mali, kizazi ana hali ingine yoyote katika ubindamu wake.

Aidha azimio linataja kwamba, kila mtu ana haki ya uhuru maisha, na usalama wa mtu. Hivyo utendaji wowote unaotaka kumlazimisha mwingine kuishi kinyume na matamanio yake au kumpa vitisho ni kutenda kinyume cha haki za binadamu. Na kwamba, hakuna mtu anayeweza kufanyishwa kazi katika hali za utumwa au utwana; utumwa na biashara yake yote ni marufuku katika kila hali. Na
hakuna mtu mwenye kuwa na mastahili ya kuteswa na aina yoyote ya ukatili, unyama au udhalilishaji au adhabu. Na kila mtu, ana haki ya kutambulika kama mtu mbele ya sheria.

Kwa maana hiyo Ibara ya 7 inasema, watu wote ni sawa mbele ya sheria na wanayo haki sawa, bila ubaguzi wowote kupata ulinzi sawa wa sheria. Wote wana haki sawa ya kulindwa dhidi ya ubaguzi na maonevu yote.

Iwapo ndivyo ilivyo, leo hii ikiwa inapita miaka 50 kwa mataifa mengi ya Afrika tangu kujipatia uhuru, na kupita kwa miaka karibia mia mbili tangu kutolewa kwa azimio la kukomesha utumwa na madhulumu yake yote, ni kipindi cha kutosha wana wa Afrika kuwa na ufahamu wa kutosha juu ya haki hizi. Ndiyo maana inashangaza kuona, watu bado wanadiriki kunyima wenzao haki msingi katika maisha. Kipindi cha miaka 50 , ni kipindi kinachotazamiwa waliozaliwa wakati huo wa uhuru, sasa wanaingia katika kundi la watu wazima, waliokomalia katika uhuru , walio elimika na kuuuishi ustaraabu huu wa uhuru tangu wakiwa watoto.

Katika ukweli wake madhulumu ya kufanyishwa kazi katika hali ya utumwa inapaswa kuwa simulizi za wakongwe na si za kizazi hiki.

Kwa kuwa madhulumu haya yanatokea katika mazingira yetu tuishimo, je kama Wakatoliki walei, tunajishughulisha kwa namna gani, kuzuia madhulumu haya , yanayofanywa na watu wachache werevu wanjanja walaghai, wanaotafuta utajiri kwa kugandamiza wengine?

Bado akilini mwetu, tunagongwa na matukio yaliyotolewa na vyombo vya habari vya Tanzania , juu wa watu wanaokwenda bara na kununua watoto na kuwasafirisha hadi Zanzibar kwa lengo la kuwapeleka mbali zaidi uarabuni na kwingineko, ambako wanatajwa kuishia katika kazi za sulubu majumbani mwa watu,wakiw wamenyiwa uhuru wao wa kutembea au kupumzika wanavyotaka.

Haya ni madhulumu makubwa yanayopaswa kukomeshwa mara moja . Ni muhimu kwa kila mmoja wetu na hasa vijana , kuhusika na utoaji wa msaada kwa yeyote anayehisi kuna mtego wa kuuuzwa au kuchukuliwa na watu asiowajua ,na hasa watoto wa kike na wa kiume pia. Kwa kuzingatia roho ya umoja na ushirikiano inayotajwa na Kanisa na Azimio la Umoja wa Mataifa, upo mshikamano wa kijamii usioweza kutenguliwa, wa kila anayezaliwa anakuwa ni sehemu ya jamii. Hivyo jamii inayo haki kamili ya kutaka maelezo kutoka kwa mzazi, pale mtoto anapotoweka kimya kimya kijijini.

Wazazi na watu wote wanapaswa kujua kwamba, hali za ajira leo hii si kama ilivyokuwa siku za nyuma. Kama ilivyo Afrika pia Ulaya na uarabuni, hakuna ajira za kueleweka. Sasa kama wenyeji wenyewe wanakosa ajira, iweje watoka mbali kwapate ajiri halali kiurahisi hivyo?

Maisha ni magumu pote duniani . Heri kubaki katika eneo lako la kuzaliwa ambako kuna mjomba na shangazi wanaoweza kukusaidia ukipatwa na matatizo, kuliko kwenda majuu asikokujua mtu.

Imeandaliwa nami TJMhella, Idhaa ya Kiswahili ya Redio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.