2013-03-16 16:49:56

Asanteni sana wanahabari, kazi yenu wameiona!


Askofu mkuu Claudio Maria Celli, Rais wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano ya Jamii, Jumamosi, tarehe 16 Machi 2013 wakati wanahabari walipokutana na Baba Mtakatifu Francis, aliwatambulisha kwa kusema kwamba, tukio hili lilikuwa limewakutanisha wanahabari kutoka katika nchi 81 waliofuatilia kwa ukaribu zaidi matukio yaliyokuwa yanatendeka hapa mjini Vatican, tangu siku ile Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita alipong'atuka kutoka madarakani hadi Baba Mtakatifu Francis alipochaguliwa na kuonekana hadharani. Kipindi chote hiki, Kanisa Katoliki limekuwa ni mdau mkuu wa vyombo vya habari kutoka sehemu mbali mbali za dunia.

Wanahabari wamefanya kazi kubwa katika kuwafikishia watu ujumbe wa kile kilichokuwa kinatendeka hapa mjini Vatican. Ni tukio ambalo watu wengi wamelifuatilia kwa hisia, mashaka na matumaini. Vyombo vya habari vimetekeleza wajibu wake kwa uhuru kamili, weledi, busara na hekima kubwa, kwa matukio haya ambayo ni muhimu sana kwa maisha na utume wa Kanisa. Utofauti wa hadhira inayokusudiwa, mahali na weledi umeviwezesha vyombo vya habari kufikisha utajiri mkubwa wa maisha na utume wa Kanisa sehemu mbali mbali za dunia.







All the contents on this site are copyrighted ©.