2013-03-15 10:36:42

WCC ina mkaribisha Baba Mtakatifu Francis katika mapambano dhidi ya changamoto za ulimwengu mamboleo


Dr. Olav Fykse Tvait, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni amemtumia salama za kiekumene Baba Mtakatifu Francis, akimpongeza kwa kuchaguliwa kwake kuliongoza Kanisa Katoliki, kielelezo kikubwa cha maisha ya Kanisa Katoliki na waamini wa madhehebu mengine pia.

Baba Mtakatifu Francis ni hujaji wa haki na amani kutoka Amerika ya Kusini; kiongozi ambaye alijitosa bila ya kujibakiza kutafuta haki jamii, akipania kuwainua maskini na wote waliokuwa wanasukumizwa pembezoni mwa Jamii. Kuchaguliwa kwake ni changamoto ya kuendeleza jitihada za kutafuta haki na amani katika Jumuiya ya Kimataifa.

Mara baada ya Maadhimisho ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, miaka hamsini iliyopita, Baraza la Makanisa Ulimwengu limeendelea kuwa na uhusiano na majadiliano ya kina na Kanisa Katoliki katika kutafuta na kujenga umoja wa Kanisa; ufahamu wa Kanisa, utume sanjari na kukoleza majadiliano ya kidini na kiekumene. Ni matumaini ya Baraza la Makanisa Ulimwenguni kwamba, uhusiano mwema kati ya pande hizi mbili utaendelezwa na kuimarishwa.

Viongozi wa Makanisa wanatambua na kuthamini mchango wa Baba Mtakatifu Francis katika masuala ya kijamii; majadiliano ya kidini na kiekumene na kwamba, uzoefu na mang'amuzi yake ya mikakati na shughuli za kichungaji yatachangia kwa namna ya pekee kabisa katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Ni matumaini ya Dr. Tveit kwamba, Makanisa yatawajibika kutoa ushirikiano kwa Baba Mtakatifu Francis, kwa kutambua kwamba, Wakristo wengi wanaishi katika nchi zinazoendelea duniani. Baba Mtakatifu anakaribishwa na Baraza la Makanisa Ulimwengu ili kuungana nao katika kupambana na changamoto za dunia.







All the contents on this site are copyrighted ©.